Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 24 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 204 2016-05-20

Name

Ussi Salum Pondeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chumbuni

Primary Question

MHE. SALUM MWINYI REHANI (K.n.y. MHE. USSI SALUM PONDEZA AMJADI) aliuliza:-
Hapo kwanza Maafisa Uhamiaji wetu walikuwa wakipelekwa kwenye Balozi zetu kufanya kazi ya kutoa viza kwa wageni wanaotaka kuja Tanzania lakini hivi sasa Maafisa hao hawafanyi tena kazi hiyo na badala yake kazi hizo zinafanywa na Maafisa wa Wizara ya Mambo ya Nje na hutoa viza hata kwa waombaji wasiotakiwa kupewa:-
(a) Je, kwa nini Maafisa hao wa Uhamiaji waliondolewa kwenye Balozi hizo?
(b) Je, ni sahihi kwa Maafisa wa Mambo ya Nje kufanya kazi za kutoa viza kwa wageni?

Name

Dr. Susan Alphonce Kolimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza, lenye sehemu mbili kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Balozi zake mbalimbali nje ya nchi na Ofisi za Wawakilishi wa Heshima (Honorary Consuls) imeendelea kutoa huduma ya viza kwa wageni mbalimbali wanaokusudia kusafiri kuja nchini Tanzania kwa madhumuni mbalimbali. Kazi ya kutoa viza hufanywa na Maafisa wa Serikali ambao wapo Ubalozini kwa nchi zenye Uwakilishi wa Kibalozi na Wawakilishi wa Heshima (Honorary Consuls) kwa maeneo ambayo Tanzania haina uwakilishi wa Kibalozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi za Balozi za Tanzania nje ya nchi huwa na Maafisa wa aina mbalimbali wakiwemo Maafisa Mambo ya Nje, Maafisa kutoka Idara ya Uhamiaji, Waambata Jeshi pamoja na Maafisa kutoka Idara mbalimbali za Serikali kwa kadri ya mahitaji ya Ubalozi husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, sehemu kubwa ya Maafisa katika Ofisi za Ubalozi huwa ni Maafisa wa Mambo ya Nje. Kutokana na Idara ya Uhamiaji kutokuwa na Maafisa Uhamiaji katika baadhi ya Balozi zake, kazi ya utoaji viza katika baadhi ya Balozi zisizo na Maafisa wa Uhamiaji hufanywa na Maafisa wa Mambo ya Nje. Kazi hiyo huongozwa na taratibu na misingi maalum ya kisheria kama ilivyoainishwa katika Sheria ya Uhamiaji, Sura ya 54 ya mwaka 2002.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majukumu ya Maafisa Uhamiaji katika Balozi hizi ni kama ifuatavyo:-
(i) Utoaji wa viza kwa wageni wanaotaka kutembelea Tanzania;
(ii) Kushughulikia pasi za kusafiri za Watanzania wanaoishi katika nchi za uwakilishi;
(iii) Kutoa hati za kusafiria za dharura kwa Watanzania walipoteza pasi zao za kusafiria au ambao wameingia nchi za uwakilishi bila pasi za kusafiria;
(iv) Kutembelea magereza zenye wafungwa ambao ni raia wa Tanzania; na
(v) Kuthibitisha uraia wa wageni ambao hufika Ubalozini na kujitambulisha kuwa ni Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upangaji wa Maafisa Uhamiaji katika Balozi zetu hufanywa na Idara ya Uhamiaji. Maafisa hao hupangwa katika Balozi zetu kulingana na mahitaji ya Idara hiyo. Mathalani Idara ya Uhamiaji iliwarudisha Bwana Sylvester Ambokile aliyekuwa Afisa Uhamiaji London na kuteuliwa kuwa Kamishna Mkuu wa Uhamiaji Makao Makuu na Bwana Johari Sururu ambaye alikuwa Afisa Uhamiaji Abu Dhabi na kuteuliwa kuwa Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar. Hivyo, jukumu la Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ni kuwezesha maafisa hawa kutekeleza majukumu yao pindi wanapokuwa vituoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kama ilivyokwishaelezwa si Balozi zote za Tanzania nje ya nchi zina Maafisa Uhamiaji. Hivyo, uwepo wa Maafisa Mambo ya Nje au Maafisa wengine wa Serikali katika Balozi hizo wanaotoa viza kwa wageni mbalimbali wanaokusudia kuja Tanzania hauna madhara yoyote kwa kuwa shughuli hiyo hufanywa kwa kuongozwa na utaratibu na misingi maalum ya kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu haina taarifa inayoonyesha kuwa kuna Maafisa Mambo ya Nje ambao wamekuwa wakitoa viza kwa waombaji wasiostahili katika Balozi zetu zilizo nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.