Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 1 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 10 2022-04-05

Name

Minza Simon Mjika

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MINZA S. MJIKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa fidia kwa Wananchi wa Simiyu wanaopakana na Hifadhi za Wanyamapori na kuathiriwa na wanyama hao?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Minza Simon Mjika, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto hiyo, Wizara imeendelea kutekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Kusimamia Utatuzi wa Migongano baina ya Binadamu na Wanyamapori wa mwaka 2020/2021 mpaka 2025 kwa kufanya yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nikufanya doria za mara kwa mara kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu. Aidha, Mheshimiwa Rais alielekeza vijengwe vituo vya askari katika maeneo ya Busega na Meatu. Mchakato wa ujenzi umeanza ambapo vituo viwili vitajengwa katika maeneo tajwa mwezi Aprili, 2022. Sambamba na hilo, maombi ya vibali vya kuajiri askari 600 yameshawasilishwa kwenye mamlaka husika.

Mheshimiwa Spika, mkakati mwingine ni kutoa mafunzo ya mbinu za kujilinda na kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu. Jumla ya Halmashauri 17 zimepatiwa mafunzo hayo. Aidha, Wizara ina namba maalum za simu kwenye kila kanda za kiutendaji ili kuwezesha wananchi kutoa taarifa za matukio ya wanyamapori bila malipo.

Mheshimiwa Spika, malipo ya kifuta jasho na kifuta machozi kwa mwaka wa fedha 2021/2022, jumla ya Sh.790,721,500 imetolewa kwa wananchi 3,598. Aidha, Wizara imepokea maombi ya malipo ya kifuta jasho na kifuta machozi kutoka wilaya mbalimbali zikiwemo Wilaya za Mkoa wa Simuyu. Kwa sasa Wizara inafanya uhakiki wa maombi kabla ya malipo kufanyika. Ahsante.