Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 22 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 190 2016-05-18

Name

Ester Amos Bulaya

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTER A. BULAYA aliuliza:-
Kumekuwepo na matukio ya mara kwa mara ya wananchi wa Vijiji vya Guta, Tairo, Nyamtwali na Njabeu kukamatwa na kuliwa na mamba; hadi swali hili linaandikwa, jumla ya watu watatu wameliwa na wengine kumi wamejeruhiwa.
Je, Serikali inajipangaje ili kuokoa maisha ya wananchi kutokana na hatari kubwa ya mamba hao?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Amos Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Vijiji vilivyotajwa na Mheshimiwa Mbunge vinapakana na Ziwa Victoria. Mazingira hayo yanasababisha kuwepo mwingiliano wa shughuli za kibinadamu na makazi ya wanyamapori kama vile mamba na viboko ambayo yanaweza kusababisha matukio ya wananchi kuuawa na kujeruhiwa na wanayama hao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu imepokea taarifa zilizowasillishwa na Halmashauri ya Wilaya ya Bunda ambazo zinaendelea kuhakikiwa, kwamba katika Kijiji cha Guta jumla ya wananchi wanne waliuawa na wengine tisa walijeruhiwa na mamba katika kipindi cha mwaka 2013 hadi 2015. Katika kipindi hicho, hakuna taarifa yoyote iliyotolewa na kupokelewa kuhusu matukio katika Vijiji vya Tairo, Nyamtwali na Njabeu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 69 cha Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009, kimempa mamlaka Mkurugenzi wa Wanyamapori kukasimu majukumu ya kushughulikia masuala ya wanyamapori wakali na waharibifu kwa Afisa aliyeidhinishwa. Aidha, Sheria imeainisha utaratibu wa kutoa taarifa za matukio kuanzia kwa Mtendaji wa Kijiji, Maafisa Wanyamapori walio karibu hadi Wizarani kwa hatua zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuokoa maisha ya wananchi kutokana na hatari ya mamba na viboko katika vijiji vilivyotajwa, Wizara yangu kupitia Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori (TAWIRA) kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Bunda itafanya tathmini ya ongezeko la mamba na iwapo itadhihirika kuwa idadi yao ni kubwa kuliko viwango vinavyokubalika, hatua stahiki zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kuweka utaratibu wa kuwavuna wanyama hao. Utaratibu huu utatumika katika maeneo yote yenye uhatarishi wa mamba na viboko. Wizara itaendelea kutoa elimu kuhusu uhifadhi, jinsi ya kujilinda na kujiepusha na wanyamapori wakali na waharibifu wakiwemo mamba pamoja na taratibu za kuwasilisha madai ya malipo ya kifuta jasho na machozi kwa wale watakaoathirika.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada hizo za Serikali, Wizara inatoa wito kwa wananchi kuendelea kuchukua tahadhari katika maeneo hatarishi hususan ambayo yamebainika kuwa na mamba au viboko na kuwasilisha taarifa za matukio haraka kwa Viongozi wa Vijiji husika na Maafisa Wanyamapori walio karibu ili kumbukumbu za matukio na hatua stahiki ziweze kuchukuliwa mapema.