Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 22 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 188 2016-05-18

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. MARGARET S. SITTA) aliuliza:-
Je, ni sababu zipi zinazoifanya Serikali yetu iridhike na utaratibu wenye usumbufu mkubwa unaowataka wakazi wa Tanzania wanaotaka kwenda Uingereza watafute visa kupitia Kenya na Afrika Kusini?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hapo awali huduma za viza zilikuwa zikitolewa na Ubalozi wa Uingereza, nchini. Ubalozi huo ulihamisha shughuli za utoaji wa viza kutoka hapa nchini kwenda nchini Kenya tarehe 1 Desemba, 2008 na kuanzia tarehe 18 Agosti, 2014 huduma hizo zimehamishiwa nchini Afrika Kusini na siyo Kenya tena.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Serikali ya Uingereza, uamuzi huo ni wa kisera na umefikiwa ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi wa Idara ya Viza na Masuala ya Uhamiaji ya Uingereza. Hivyo, mchakato wa utoaji visa za Uingereza unafanyika kikanda. Kwa mantiki hiyo, maombi yote ya viza kutoka
NAKALA YA MTANDAO (ONLINE DOCUMENT)
15
nchi zote za Afrika Mashariki na Kati, yanafanyiwa kazi katika Ubalozi wa Uingereza, nchini Afrika ya Kusini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, waombaji wa viza hapa nchini wanatakiwa kuwasilisha maombi yao na nyaraka zinazohitajika katika Kituo cha Kuombea Viza, (Visa Application Center) kilichopo Viva Tower Dar es Salaam. Kituo hicho ndicho chenye jukumu la kusafirisha maombi yao kwenda Afrika ya Kusini na kurejesha nyaraka husika kwa waombaji nchini. Mwombaji halazimiki kufuata huduma hiyo nchini Afrika ya Kusini.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Ubalozi wa Uingereza Nairobi unashughulikia maombi machache ya Visa (restricted number of applications) kwa viongozi wa Serikali na watendaji wengine wenye pass za Kidiplomasia hasa katika hali ya dharura. Maombi hayo yanapaswa kupelekwa moja kwa moja Ubalozi wa Uingereza Nairobi na waombaji wenyewe au kupitia Ubalozi wa Tanzania Nairobi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania wenzangu kwamba zoezi la utoaji visa lina utaratibu wake na moja ya taratibu hizo ni kwamba nchi inayotoa visa ina uhuru wa kuamua ni wapi itatolea visa hizo. Kwa mantiki hiyo, hata Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupitia Balozi zake zilizopo nje, inazo taratibu zake za kutoa visa kwa wageni wanaotembelea Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema Watanzania ambao wangependa kutembelea nchi ya Uingereza wakazingatia taratibu zilizowekwa za nchi hiyo katika maombi ya visa ikiwemo kuomba visa mapema, kuwasilisha nyaraka zote muhimu na taarifa sahihi ili kuepuka usumbufu usio wa lazima.