Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 21 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Ofisi ya Rais TAMISEMI. 177 2016-05-17

Name

Juma Selemani Nkamia

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chemba

Primary Question

MHE. JUMA S. NKAMIA aliuliza:-
Wakulima wengi wa Wilaya ya Chemba wamefukuzwa katika mashamba yao Wilayani Kiteto licha ya kufuata taratibu na kudaiwa kuwa eneo hilo ni hifadhi.
Je, Serikali ipo tayari kufuta uamuzi uliotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Manyara wa kuwazuia wakulima hawa ili kuondoa mgogoro huu wa muda mrefu?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juma Selemani Nkamia, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, tamko lililotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Manyara liliwahusu wakulima waliokuwa wavamizi katika eneo la Hifadhi ya Wanyamapori Makame kutoka Wilaya ya Kiteto, Babati, Chemba, Kondoa na Mkoa wa Iringa, waliokuwepo wakiendesha shughuli za kilimo katika hifadhi kinyume cha sheria.
Mheshimiwa Spika, uamuzi huo ulitolewa kufuatia Azimio la kikao cha pamoja cha Kamati ya Ulinzi na Usalama za Wilaya ya Kiteto na Chemba kilichokaa tarehe 12 Novemba, 2015. Kikao hicho kiliwashirikisha viongozi wa Vijiji vitano vinavyounda Mamlaka ya Hifadhi (WMA) ambavyo ni Ngobolo, Katikati, Ndedo, Ikshubo na Makame, pamoja na wawakilishi wa wakulima 10 kutoka kila Wilaya.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa sheria hairuhusiwi shughuli yoyote ya kibinadamu, iwe kilimo, ufugaji au makazi kuendeshwa katika hifadhi. Naomba kutoa wito kwa wananchi kuzingatia sheria za nchi ili kuepuka migogoro katika jamii. Aidha, Serikali za vijiji zinakumbushwa kusimamia vizuri sheria ya ardhi namba tano ya mwaka 1999 ambayo imeweka utaratibu wa kufuata kwa mtu atakayehitaji kupata ardhi kwa matumizi mbalimbali. Lengo ni kuzuia migogoro ya ardhi isiyokuwa ya lazima ambayo kwa sehemu kubwa inatokana na kutozingatia Sheria ya Ardhi.