Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 20 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 174 2016-05-16

Name

Dr. Immaculate Sware Semesi

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI aliuliza:-
(a) Je, Serikali inasafirisha nje ya nchi mbao na magogo kiasi gani kwa mwaka?
(b) Je, ni nchi gani inaongoza kwa kununua mbao na magogo kutoka Tanzania?
(c) Je, ni fedha za kigeni kiasi gani zimepatikana kutokana na mauzo ya magogo na mbao nje ya nchi kwa kipindi cha mwaka 2010 - 2015?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Immaculate Sware Semesi, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni ya 50 ya Kanuni za Sheria ya Misitu Namba 14 ya mwaka 2002, inakataza usafirishaji wa magogo kwenda nje ya nchi. Aidha, Kanuni hiyo hairuhusu uuzaji nchi za nje wa mbao zenye unene unaozidi inchi sita. Kanuni hii na sheria vinaweka zuio ili kutoa fursa ya kukuza viwanda vya ndani ya nchi na ajira kwa Watanzania katika kupasua mbao na utengenezaji wa samani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015 jumla ya mita za ujazo 333,404.91 za mbao chini ya inchi sita ziliuzwa na kusafirishwa kwenda nchi za nje.
Aidha, kwa mujibu wa takwimu nchi ya India inaongoza kwa kununua mbao kutoka Tanzania ambapo katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015 jumla ya meta za ujazo 210,968.07 zilisafirishwa kwenda India, ikifuatiwa na nchi ya China ambayo ilinunua mita za ujazo 68,337.04.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015 jumla ya fedha zilizopatikana ni shilingi 269,985,300,000 kutokana na mauzo ya mbao nchi za nje. Aidha, hakuna kiasi cha fedha kilichopatikana kutokana na mauzo ya magogo kwa kuwa biashara ya magogo kwa mujibu wa sheria haikufanyika.