Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 13 Water and Irrigation Wizara ya Maji 157 2022-02-17

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itasambaza maji katika Vijiji vya Mwanjoro, Jinamo, Mbushi na Witamihya Wilayani Meatu baada ya ujenzi wa Bwawa la Mwanjoro kukamilika?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vijiji vya Mwanjoro, Jinamo, Mbushi na Witamihya kwa sasa vinapata huduma ya maji kwa wastani wa asilimia 24 kupitia visima vifupi 13.

Mheshimiwa Spika, bwawa la Mwanjolo lilikamilika mwishoni mwa mwaka 2018 likiwa na lengo la kuhudumia vijiji vya Jinamo, Mbushi na Mwanjoro, lakini katika utafiti uliofanyika hivi karibuni bwawa hilo limeonekana kupungua kina kutokana na kujaa kwa mchanga unaosababishwa na kunyweshea mifugo na changamoto ya uharibifu wa mazingira iliyopelekea pia kuathiri ubora wa maji hayo.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kuwa Bwawa la Mwanjolo linatumika kusambaza maji vijiji vya Mwanjoro, Jinamo, Mbushi. Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 itatenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa Bwawa la Mwanjolo ambapo ukarabati huu utahusisha kuongeza kwa kina cha bwawa, kujenga kingo za bwawa ambazo kwa sasa zimechakaa. Kujenga miundombinu ya kuzuia mchanga kuingia katika Bwawa (sand trap) pamoja na upandaji wa miti na nyasi ili kuzuia mmomonyoko wa ukuta. Pia katika bajeti hiyo Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kujenga miundombinu ya kunyweshea maji mifugo ili wafugaji wasiweze kuingiza mifugo yao kwenye bwawa na mwisho wananchi wa maeneo haya watapewa elimu ya utunzaji wa vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, mpango wa muda mrefu vijiji hivi pia vitaweza kunufaika na mradi mkubwa unaotarajia kujengwa katika Mkoa wa Simiyu kupitia program ya mabadiliko ya tabia ya nchi maana vijiji hivi vya Mwanjoro vipo umbali wa kilomita 12 toka kwenye eneo la ujenzi wa bomba kuu.