Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 13 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 154 2022-02-17

Name

Mwanaisha Ng'anzi Ulenge

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE aliuliza: -

Je, nini kauli ya Serikali kutokana na mkanganyiko uliotokea kuhusu fidia katika barabara ya Tanga – Pangani?

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Mwanaisha Ng’anzi Ulenge, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Tanga – Pangani yenye urefu wa kilomita 50 ni sehemu ya barabara ya Bagamoyo kuanzia Makurunge – Saadani – Pangani hadi Tanga ambayo ina urefu wa kilomita 256. Awali Benki ya Maendeleo ya Afrika ilionesha nia ya kufadhili barabara yote ya Bagamoyo kuanzia Makurunge – Saadani – Pangani hadi Tanga urefu wa kilomita 256.

Mheshimiwa Spika, aidha, mfadhili alitoa sharti la kulipia fidia kwa mali zote zitakazoathiriwa na mradi ndani na nje ya eneo la hifadhi ya barabara. Hivyo, uthamini wa mali zitakazoathiriwa na mradi ulifanyika kwa kuzingatia sharti hilo. Wananchi walifahamishwa kwenye mikutano ya uelimishaji umma na kujulishwa kuwa endapo mfadhili hataendelea na nia hiyo na Serikali ikajenga kwa fedha za ndani, wale wenye mali zilizopo ndani ya eneo la hifadhi ya barabara hawatalipwa fidia.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hiyo, na kwa kutochelewesha mradi, Serikali ilianza ujenzi kwa sehemu ya Tanga, hadi Pangani urefu wa kilomita 50 kwa kutumia fedha za ndani.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Barabara Na. 13 ya Mwaka, 2017 ujenzi wa aina yoyote hauruhusiwi ndani ya eneo la hifadhi ya barabara. Hivyo, wananchi waliofanya maendelezo ndani ya eneo hilo hawastahili kulipwa fidia.

Mheshimiwa Spika, kwa kufuata matakwa ya sheria za nchi wale wote ambao walikuwa ndani ya eneo la hifadhi ya barabara, hawakustahili kulipwa fidia na waliondolewa kwenye orodha ya malipo kabla ya taarifa ya fidia kuwasilishwa kwa Mthamini Mkuu wa Serikali. Ahsante.