Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 11 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 130 2022-02-15

Name

Dr. Joseph Kizito Mhagama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Madaba

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapunguza gharama za vibali vya kuanzisha biashara ya kuuza pembejeo za kilimo Vijijini ambapo TFRA, TOSCI na TPRI huchukua takribani shilingi 600,000 kabla mfanyabishara hajaingiza mtaji dukani?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama, Mbunge wa Madaba, kama ifuatavyo: -

Mhashimiwa Mwenyekiti, watoa huduma wa pembejeo ikiwemo mbegu, viuatilifu na mbolea katika ngazi zote, wanatakiwa wawe na uelewa mpana wa huduma wanazozitoa. Gharama za kuanzisha biashara ya pembejeo hizo hutokana na mafunzo maalum yanayotolewa na taasisi husika kwa lengo la kujenga uwezo kwa Mawakala na Kampuni za pembejeo ili kutoa huduma stahiki kwa wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Mbegu Na. 18 ya mwaka 2003 na marekebisho yake ya mwaka 2014 pamoja na Kanuni za mwaka 2007 na marekebisho ya mwaka 2017; hakuna tozo za kuanzisha biashara ya mbegu, isipokuwa kuna ada ya mafunzo ambayo ni shilingi 150,000 kwa kampuni na wazalishaji/ mawakala wasambazaji wa mbegu bora. Aidha, kwa wazalishaji wa mbegu za kuazima (Quality Declared Seed) hutozwa shilingi 50,000 kwa ajili ya mafunzo maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa viuatilifu na ukaguzi wa eneo la duka linalofunguliwa ni kiasi cha shilingi 172,500 na shilingi 350,000 hutozwa kwa ajli ya mafunzo. Malipo haya ni kwa mujibu wa Sheria ya Afya ya Mimea ya mwaka, 2020. Kwa upande wa Mamlaka ya Mbolea Tanzania - TFRA hakuna tozo kwa mfanyabiashara anayetaka kuanzisha duka la kuuza mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika kuboresha mazingira ya wazalishaji na wasambazaji wa pembejeo ilifuta tozo na ada mbalimbali kwa upande wa mbegu jumla ya tozo 12 zilizokuwa zikigharimu jumla ya shilingi 180,500 zilifutwa. Vilevile Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea ilifuta tozo nne zilizokuwa na shilingi 2,240,000. Hivyo, nitoe wito kwa wafanyabishara wenye nia ya kuanzisha maduka ya pembejeo kujitokeza na kuanzisha maduka hayo ili kusogeza huduma hiyo karibu na wakulima. (Makofi)