Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 11 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 127 2022-02-15

Name

Capt. Abbas Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Fuoni

Primary Question

MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI aliuliza: -

Je, Serikali imewekeza kiasi gani cha fedha katika ununuzi wa ndege 11 za ATCL na ni lini uwekezaji huo utarudisha fedha zilizowekezwa?

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Answer

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu, nikiwa kwenye nafasi hii ya Naibu Waziri kwenye Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, kwenye Sekta ya Uchukuzi, napenda nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kupitia mtumishi wake Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuniona na kuniteua kwamba nimsaidie kwenye Sekta hii ya Uchukuzi. Naahidi kwamba nitafanya kadri ya uwezo wa Mwenyezi Mungu lakini pia kwa nguvu, weledi na uadilifu mkubwa. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizi, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi, napenda nijibu swali la Mheshimiwa Abbas Ali Mwinyi, Mbunge wa Fuoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Ndege za Serikali kwa maana Tanzania Government Flight Agency-TGFA imewekeza kiasi cha Shilingi trilioni 1.44 katika ununuzi wa ndege 11 ambapo, kati hizo, ndege mbili ni za safari za masafa marefu aina ya Boeing 787-8 Dreamliner, Ndege nne ni za safari za masafa ya kati aina ya Airbus A220- 300 na ndege Tano za safari za masafa mafupi aina ya De Havilland Dash 8 Q400.

Mheshimiwa Spika, biashara ya usafiri wa anga faida yake haitokani na uendeshaji wa ndege zinazotumiwa na Kampuni katika kutoa huduma zake tu, bali hutokana pia na mchango wake katika ukuaji wa sekta nyingine za kiuchumi kama utalii, viwanda, madini, kilimo, mifugo, uvuvi, biashara, kuitangaza nchi kimataifa na kuwezesha usafirishaji wa abiria na mizigo ndani na nje ya nchi. Aidha, ATCL imeleta ushindani mkubwa na kuzuia upandaji wa nauli katika usafiri wa anga.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuchangia kwenye ukuaji wa Sekta nyingine, ATCL imeendelea kujiendesha kibiashara na kupunguza utegemezi kwa Serikali kwa kuanzisha vitengo vya kibiashara ambavyo vinasimamia huduma za matengenezo ya ndege, huduma za chakula cha abiria wa ndani ya ndege na huduma za abiria na mizigo kwa maana grounds handling services. Uwepo wa vitengo vinavyotoa huduma hizo umewezesha ATCL kupunguza gharama za uendeshaji. Mashirika mengine ya ndege yanayotumia utaratibu huu ni pamoja na Shirika la Ndege la Ethiopia. Ahsante. (Makofi)