Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 11 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu 120 2022-02-15

Name

Anton Albert Mwantona

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rungwe

Primary Question

MHE. ANTON A. MWANTONA aliuliza: -

Je, nini mchango wa Serikali katika kuwawezesha vijana zaidi ya 100 waliomaliza Vyuo vikuu ambao wapo tayari kwa ajili ya kujiajiri katika kilimo Wilayani Rungwe kupitia Ofisi ya Mbunge?

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WATU WENYE ULEMAVU (MHE. PATROBASS P. KATAMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Rungwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kutambua umuhimu wa vijana katika kukuza uchumi na kuleta maendeleo ya jamii nchini, imeendelea kuweka mazingira wezeshi ili vijana waweze kuanzisha na kuendesha shughuli zao za kujitegemea kwa kutumia fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali. Baadhi ya fursa hizo ni kama ifuatavyo: -

(i) Utengaji wa maeneo maalumu kwa ajili ya shughuli za vijana za kiuchumi zikiwemo shughuli za kilimo. Halmashauri zote nchini zimeagizwa kutenga maeneo hayo, ambapo Halmashauri ya Rungwe imetenga Ekari 88.9 kwa ajili ya shughuli za kilimo, viwanda na masoko.

(ii) Mafunzo ya kilimo cha kisasa kwa kutumia teknolojia ya kitalu nyumba kwa ajili ya mazao ya muda mfupi (mbogamboga). Mafunzo hayo yamenufaisha vijana 98 wa Halmashauri ya Rungwe kati yao 15 wamejifunza namna ya kujenga vitalu nyumba.

(iii) Mikopo isiyo na riba ya 4% iliyotengwa na Halmashauri hiyo ya Rungwe kwa mwaka wa fedha 2021/ 2022 imetenga zaidi ya shilingi milioni 133.7 kwa ajili ya vijana.

(iv) Mikopo yenye riba nafuu ikiwemo Mifuko na Program za uwezeshaji wananchi kiuchumi, ukiwemo Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ili kuwawezesha vijana kuanzisha na kuendeleza miradi mbalimbali katika sekta ya kilimo katika eneo hilo la Jimbo la Rungwe.

(v) Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo imeanzisha Mpango uitwao “Building a Better Tomorrow” unaowalenga Vijana wahitimu na wasio na kazi wajiingize katika kufanya shughuli katika sekta ya kilimo. Katika mpango huu, Ofisi ya Waziri Mkuu itakuwa na jukumu la kuwapatia mafunzo vijana. Vile vile Wizara ya Kilimo itakuwa na wajibu wa: kwanza, kutoa ardhi; pili, kuweka mitaji na kuwatafutia mitaji vijana hawa; na tatu, kuweka miundombinu katika mashamba ambayo yatakuwa yametengwa ya Agro Parks/Blocks pamoja na kuwaunganisha na masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge kupitia ofisi yake awashauri na kuwahimiza vijana wa Rungwe waliohitimu Vyuo Vikuu kuzingatia fursa zinazotolewa na sisi tutaendelea kumpa ushirikiano popote atakapohitaji ili kuweza kuwaunganisha vijana na kuwaweka katika kazi. Ahsante.