Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 8 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 90 2022-02-10

Name

Lucy John Sabu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCY J. SABU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka Dirisha Maalum la Vijana kwenye kila Benki za Serikali nchini ili kuwawezesha vijana kupata mitaji na mikopo yenye riba nafuu?

Name

Hamad Hassan Chande

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kojani

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy John Sabu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania inatekeleza sera na mikakati mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha kuwa riba za mikopo zinashuka ili kuwezesha makundi yote likiwemo kundi la vijana yanapata mikopo yenye riba nafuu na kuweza kushiriki vyema katika shughuli za kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Benki za Serikali zinatoa huduma za mikopo kwa makundi yote likiwemo kundi la vijana kwa kuzingatia taratibu za utoaji mikopo za mabenki ambapo kwa wale wenye vigezo hupatiwa mikopo bila usumbufu wowote.

Mheshimiwa Spika, aidha, kwa kutambua umuhimu wa kundi la vijana katika suala zima la upatikanaji wa mikopo yenye riba nafuu kwa ajili ya kuwawezesha kufanya shughuli za kiuchumi, Serikali ilianzisha programu maalum ya utoaji mikopo ya uwezeshaji yenye riba nafuu kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa mujibu wa Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura 290 pamoja na Kanuni zake za mwaka 2019 ambapo halmashauri zote zinatakiwa kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya kutoa mikopo kwa makundi hayo. Vijana wengi nchini wameendelea kunufaika na mikopo hiyo hadi sasa.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuhakikisha vijana wote wanaokidhi vigezo na masharti ya kupata mikopo wanapatiwa mikopo ili kuendesha shughuli zao na hatimaye waweze kuwa na mchango kwenye ukuaji wa uchumi na pato la Taifa letu. Ahsante.