Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 7 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 79 2022-02-09

Name

Florent Laurent Kyombo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Primary Question

MHE. FLORENT L. KYOMBO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawatambua watu wenye haki ya Uraia ili wapate Vitambulisho vya Taifa pamoja na kuwapa Uraia watu ambao siyo raia lakini wameishi nchini kwa zaidi ya miaka kumi na tano?

Name

Sagini Jumanne Abdallah

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Butiama

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kuwa na afya na leo kushiriki kwenye kikao cha Bunge.

Mheshimiwa Spika, pia nimshukuru Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kuniamini kuwa mmoja wa wasaidizi wake katika nafasi ya Naibu Uwaziri. Ahadi yangu kwake ni kutekeleza majukumu haya kwa uadilifu, uaminifu na bidIi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, nikupongeze kwa kuchaguliwa kwa kura zote kuwa kiongozi wetu wa Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo sasa, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Florent Laurent Kyombo, Mbunge wa Nkenge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na zoezi la kuwatambua na kuwapatia vitambulisho wale wote wanaostahili. Aidha, zoezi hili ni endelevu kwa kuwa kila mwaka idadi ya watu wanaofikisha umri na vigezo vya kutambuliwa na kusajiliwa inaongezeka. Aidha, idadi ya wageni wakazi na wakimbizi wanaoingia nchini imekuwa ikiongezeka na hivyo kuhitaji kusajiliwa na kutambuliwa ili kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na utaratibu wa kuwapatia uraia wa Tanzania (Tajnisi) wageni ambao wanaomba uraia wa Tanzania ikiwa wamekidhi sifa na vigezo vya kutajnisiwa uraia kwa mujibu wa Sheria ya Uraia Sura ya 357, Toleo la Mwaka 2002 na Kanuni zake. Ahsante.