Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 7 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 78 2022-02-09

Name

Esther Edwin Maleko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER E. MALLEKO aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuanzisha makongamano ya Kimataifa ili kukuza utalii wa Mlima Kilimanjaro?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, lakini kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuendelea kutuamini mimi na Mheshimiwa Waziri kuendelea kuhudumu Wizara hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, kipekee nikupongeze wewe binafsi kwa kuteuliwa kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; tunakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, sasa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau imekuwa ikiendelea kuutangaza Mlima Kilimanjaro kwa kutumia mbinu mbalimbali zikiwemo: -

(a) Onesho la Utalii la Kimataifa la Kilifair linalofanyika Mjini Moshi Mwezi Juni kila mwaka;

(b) Mbio za Kilimanjaro (Kilimanjaro Marathon) zinazofanyika Mkoani Kilimanjaro mwezi Februari kila mwaka;

(c) Kushiriki makongamano mbalimbali ya kimataifa ikiwemo WTM – London, ITB - Ujerumani, Fitur-Hispania na Expo - 2020 Dubai;

(d) Kushiriki makongamano ya kimataifa yanayolenga kuimarisha uhifadhi na kutangaza utalii wa Mlima Kilimanjaro likiwemo Kongamano la Milima Mirefu Duniani (International Mountains Alliance - ITA);

(e) Mlima Kilimanjaro ni moja ya eneo la urithi wa dunia ambapo kupitia mikutano mbalimbali ya UNESCO Mlima huo hutangazwa;

(f) Kuwatumia watalii wanaofika Tanzania kama mabalozi wa kuutangaza Mlima Kilimanjaro;

(g) Kuendelea kutumia matukio muhimu ya Kitaifa kama sherehe za Uhuru kuhamasisha jamii kupanda Mlima Kilimanjaro; na

(h) Kuandaa na kushiriki katika Onesho la Kwanza la Kimataifa la Utalii la Jumuiya ya Afrika Mashariki lilofanyika Jijini Arusha ili kutangaza vivutio vya utalii ikiwemo Mlima Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kubuni mikakati zaidi ya kuutangaza Mlima Kilimanjaro kwa maslahi mapana ya nchi. Ahsante.