Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 5 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 47 2022-02-07

Name

Noah Lemburis Saputi Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Magharibi

Primary Question

MHE. NOAH L. S. MOLLEL aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itayachukua Mashamba Pori yasiyoendelezwa kwa Shughuli iliyokusudiwa yakiwepo Mashamba ya Aghakan, Lucy Estate na Gomba Estate na kuyagawa kwa Wananchi?

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kama ilivyo ada waliyofanya wenzangu naomba kabla sijajibu swali nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniamini na kunichagua mimi na mwenzangu Mheshimiwa Dkt. Angelina Mabula kuwa katika Wizara hii ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi; ahadi yangu kwake na kwa viongozi wote wa juu yetu ni kwamba hatutowaangusha tutafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kwa ruhusa yako nijibu swali la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Arumeru Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu Mbunge wa Arumeru Magharibi kama ifuatavyo. Kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi, Sura ya 113, hatua za ubatilishaji wa milki nchini hutekelezwa ikiwa mmiliki wa shamba au kiwanja amekiuka masharti ya umiliki yaliyoainishwa kisheria.

Mheshimiwa Spika, Shamba la Agakhan kwa sasa lipo ndani ya eneo la mpangomji ambalo limeingizwa kwenye Mpango Kabambe wa uendelezaji wa Jiji la Arusha. Kwa kuzingatia mpango huo, eneo la shamba hilo limepangwa kuendelezwa kwa matumizi mbalimbali ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Chuo Kikuu, eneo la biashara na makazi. Mmiliki wa eneo hilo alipaswa kuendeleza kwa kuzingatia mpango huo. Kutokana na kubadilika kwa mpango wa matumizi ya eneo hilo, Serikali ipo katika mazungumzo na mmiliki ili kuona namna bora ya kutekeleza mpango huo.

Mheshimiwa Spika, shamba la Gomba Estate ni miongoni mwa mashamba ambayo wamiliki walichukua mikopo na kushindwa kurejesha kwa hiyo shamba hilo kwa sasa lipo chini ya uangalizi wa taasisi ya benki ya Standard Chartered na Shirika la NSSSF. Ili kutatua changamoto ya urejeshaji wa mkopo, Serikali kwa kushirikiana na wamiliki na taasisi tajwa imeanza zoezi la kupanga, kupima ardhi husika ili kupata viwanja vitakavyouzwa ili mkakati wa kurejesha mkopo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu shamba la Lucy Estate, miliki ya shamba husika ilibatilishwa mwaka 1999 kutokana na kukiukwa kwa masharti ya umiliki. Hata hivyo, mmiliki wa shamba hakukubaliana na hatua hiyo na hivyo alifungua shauri Na. 50/2015 katika Mahakama Kuu ya Arusha dhidi ya Serikali kupinga ufutaji huo. Baada ya majadiliano ya kisheria, ilikubaliwa kwamba aliyekuwa mmiliki alipwe fidia ya maendelezo yaliyokuwepo. Hivyo, Serikali inaandaa mpango wa matumizi wa shamba hilo kwa ajili ya matumizi mbalimbali na sehemu ya shamba husika itatumika kupata fedha kwa ajili ya fidia.