Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 5 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu 40 2022-02-07

Name

Dr. Thea Medard Ntara

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. THEA M. NTARA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza ajira kwa Wahitimu wa Vyuo Vikuu hasa katika Sekta ya Kilimo kwa kuwa mikopo ya Elimu ya Juu imewezesha wanafunzi wengi kuhitimu?

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Thea Medard Ntara Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kuwa ajira kwa wahitimu wa Vyuo Vikuu zinaongezeka hususan katika sekta ya kilimo, Serikali inatekeleza mipango ifuatayo: -

(i) Mpango wa Taifa wa Kukuza Ujuzi nchini ambao unatoa mafunzo ya ujuzi na uzoefu katika kilimo cha kisasa cha kutumia teknolojia ya vitalu nyumba. Kupitia mpango huo, hadi sasa jumla ya vijana 12,580 wakiwemo wahitimu wa fani ya kilimo wamepatiwa mafunzo ili waweze kujiajiri;

(ii) Mpango wa mafunzo ya uzoefu wa kazi (internship) kwa wahitimu wa elimu ya juu nchini kupitia waajiri wa ndani na nje ya nchi, ambapo jumla ya wahitimu 6,624 wamepatiwa mafunzo husika;

(iii) Mpango wa Vituo vya Uatamizi kwa Wahitimu (Incubation Centres) ambao tayari umeanza kutekelezwa katika Mikoa ya Morogoro na Pwani. Hadi sasa, jumla ya wahitimu 1,000 wamepatiwa mafunzo ya uanzishaji wa shughuli za kilimo na ujasiriamali;

(iv) Mpango wa kilimo cha vizimba (Block Farming), ambapo tayari wahitimu 39 wamepatiwa fursa ya kuanzisha shughuli za kilimo katika mashamba mbalimbali nchini;

(v) Mpango wa mafunzo ya uzoefu wa kazi kwa wahitimu, ambapo Serikali kwa kushirikiana na Ushirika wa Wahitimu wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUGECO) imewawesha wahitimu 703 kwenda nchini Israel na Marekani kupatiwa mafunzo katika kilimo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mipango hiyo, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo imeanzisha Mpango mpya uitwao ‘Building a better Tomorrow’’ unaowalenga vijana wahitimu na wasio wahitimu. Katika mpango huu, Ofisi ya Waziri Mkuu itakua na jukumu la kuwapatia mafunzo vijana hao na Wizara ya Kilimo itakua na wajibu wa kutoa ardhi, mitaji, kuweka miundombinu katika mashamba tengwa ya Agro Parks/Blocks pamoja na kuwaunganisha na masoko. Ahsante.