Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 3 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 25 2022-02-03

Name

Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Primary Question

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani mahsusi wa kuhakikisha vijana wote wanaoomba mikopo ya Elimu ya Juu wanapata mikopo hiyo kama walivyoomba?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Muleba Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kugharamia utoaji wa mikopo ya wanafunzi wa Elimu ya Juu kwa kuzingatia sheria, taratibu, kanuni na miongozo iliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kuwa kila mwanafunzi wa Elimu ya Juu mhitaji anapata mkopo kwa ajili ya kugharamia masomo yake. Katika kutimiza azma hiyo, Serikali imekua ikiongeza fedha za bajeti ya mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu kila mwaka. Kwa mfano, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali ilitoa kiasi cha shilingi bilioni 570 kwa ajili ya mikopo ya wanafunzi wa Elimu ya Juu ikiwa ni ongezeko la bilioni 106 kutoka bilioni 464 ya mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ongezeko hilo la fedha za bajeti, wanufaika wa mikopo ya Elimu ya Juu wamekuwa wakiongezeka mwaka hadi mwaka, ambapo katika mwaka 2021/2022 wanafunzi wanufaika wa mikopo ya Elimu ya Juu walikua 176,617 ikiwa ni ongezeko la wanafunzi 27,228 kutoka wanafunzi 149,389 wa mwaka 2020/ 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuongeza fedha za mikopo ya wanafunzi wa Elimu ya Juu kulingana na ongezeko la fedha katika bajeti yake ili kuhakikisha vijana wote wanaoomba mikopo ya Elimu ya Juu wanapata mikopo hiyo kama walivyoomba. Ahsante sana.