Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 2 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 15 2022-02-02

Name

Khadija Shaaban Taya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. KHADIJA S. TAYA aliuliza: -

Je, ni upi mgawanyo wa vitabu 812 vya nukta nundu vilivyotolewa katika Mpango wa Fedha za Mapambano dhidi ya UVIKO 19?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami nichukue fursa hii adhimu na adimu kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu alitupa kibali cha kukutana katika eneo hili kwa siku ya leo. Shukrani ya pili nimpelekee Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu, Mama Samia Suluhu Hasan kwa kuendelea kuniamini na kutuamini sisi, mimi na Profesa Mkenda kuweza kumsaidia katika eneo la Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayasi na Teknolojia, kujibu swali la Mheshimiwa Khadija Shaaban Taya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa vitabu vya Nukta Nundu kwa lengo la kuwawezesha wanafunzi wasioona kushiriki kikamilifu katika mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia mahitaji ya wanafunzi wasioona wapatao 514 wanaosoma katika shule za sekondari nchini, Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19 ilitenga shilingi milioni 704 kwa ajili ya kuchapa jumla ya nakala 18,200 za vitabu kwa ajili ya wanafunzi wasioona vya masomo yote ya sekondari, ambapo nakala 9,100 ni vitabu vya nukta nundu na nakala 9,100 ni vitabu vya michoro.

Mheshimiwa Spika, uchapaji wa vitabu hivyo upo katika hatua za mwisho na utakapokamilika vitasambazwa katika mikoa yote kulingana na mahitaji. Aidha, Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum katika mikoa yote wakiwemo wanafunzi wasioona. Nakushukuru.