Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 5 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 57 2021-11-08

Name

Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaondoa kabisa utaratibu wa kununua mazao kwa mkopo ambao unaendelea kutumiwa na baadhi ya Taasisi jambo ambalo linasababisha manung’uniko kwa Wakulima?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomari Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) na Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko ni Taasisi za Serikali pekee chini ya Wizara ya Kilimo ambazo imekuwa ikizitumia kuchochea soko la mazao ya wakulima hasa mazao ya nafaka. Katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali kupitia NFRA na CPB imetumia jumla ya bilioni 119 kwa ajili ya ununuzi wa mazao ya nafaka ambayo yatauzwa katika masoko ya ndani na nje.

Mheshimiwa Spika, hadi mwezi Oktoba, 2021 NFRA imetumia jumla ya bilioni 37 kununua jumla ya tani 75,000 za mahindi na CPB imetumia jumla ya bilioni 12 kwa ajili ya tani 27,000 za mahindi na ununuzi unaendelea. Aidha, ununuzi huo umefanyika katika Mikoa ya Ruvuma, Njombe, Songwe, Rukwa, Katavi, Shinyanga, Arusha na Dodoma.

Mheshimiwa Spika, NFRA na CPB hazitumii utaratibu wa kukopa wakulima wa nafaka kwani, zimekuwa zikinunua nafaka kutoka kwa wakulima na vikundi vya wakulima na kufanya malipo mara baada ya mapokezi ya nafaka katika vituo vya ununuzi. Katika msimu wa 2021/2022 taasisi hizi zinaendelea na ununuzi wa nafaka kutoka kwa wakulima na vikundi vya wakulima kwa utaratibu wa malipo ya fedha taslimu na si kwa njia ya kuwakopa wakulima.