Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 5 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Waziri Mkuu: Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu 49 2021-11-08

Name

Dr. Thea Medard Ntara

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTER A. BULAYA K.n.y. MHE. DKT. THEA M. NTARA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza ajira kwa wahitimu wa Vyuo Vikuu hasa katika sekta ya kilimo kwa kuwa mikopo ya elimu ya juu imewezesha wanafunzi wengi kuhitimu?

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCAL P. KATAMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Thea Medard Ntara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha ajira kwa wahitimu wa Vyuo Vikuu zinaongezeka hususan katika sekta ya kilimo, Serikali imetekeleza mipango ifuatayo: -

(i) Kutoa mafunzo ya kilimo cha kisasa kupitia programu ya kukuza ujuzi nchini, ambapo jumla ya vijana 12,580 katika Mikoa 17 nchini, wakiwemo wahitimu wa fani ya kilimo wamepatiwa mafunzo ya kilimo cha kisasa na sasa wapo tayari kuanza biashara ya kilimo na kutumia teknolojia na ujuzi wa kitalunyumba.

(ii) Kuwezesha wahitimu kupata uzoefu wa kazi nje ya nchi (internship), ambapo Serikali kwa kushirikiana na Ushirika wa Wahitimu wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUGECO), wamewezesha wahitimu 703 kwenda nchini Israeli na Marekani. Kati ya hao, wahitimu 311 wamerudi nchini na wamejiajiri katika maeneo mbalimbali nchini.

(iii) Kupitia Benki ya TADB na mikopo ya Halmashauri, baadhi ya wahitimu waliopatiwa mafunzo nje ya nchi wamepatiwa mikopo ya jumla ya Shilingi Milioni 170 na wanaendelea na shughuli hizo.

(iv) Kupitia Vituo vya Uatamizi kwa wahitimu (Incubator Centres) katika Mikoa ya Morogoro na Pwani, wahitimu 1,000 wamepatiwa mafunzo ya uanzishaji shughuli za kilimo na ujasiriamali na;

(v) Kupitia kilimo cha vizimba (block farming), wahitimu 39 wamepatiwa fursa ya kuanzisha shughuli za kilimo. Kati ya hao, wahitimu 30 wamepatiwa fursa ya kushiriki katika shamba la hekari 1,500 lililopo Mkoani Morogoro Mvomero. Aidha, wahitimu Tisa wamepatiwa fursa ya kushiriki katika shamba la kahawa Mkoani Songwe.

Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha wahitimu wengi zaidi wanaendelea kuwezeshwa kuajirika lakini pia kujiajiri, kupitia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa, Serikali imetenga zaidi ya Shilingi bilioni 54 ili kuwawezesha wahitimu 1,500 kupata mafunzo ya uzoefu wa kazi ikiwemo fani ya kilimo. Ahsante. (Makofi)