Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 3 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 35 2021-11-04

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kugharamia matengenezo ya Reli ya TAZARA ambayo miundombinu yake imechakaa na ni muhimu sana kwa uchumi wa Tanzania na hata nchi jirani za SADC?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mamlaka ya Reli Tanzania na Zambia (TAZARA) ilianzishwa kwa mujibu wa Sheria ya TAZARA Na. 23 ya mwaka 1975 iliyorekebishwa kwa Sheria ya TAZARA Na. 4 ya mwaka 1995. Reli hiyo inamilikiwa kwa uwiano wa hisa hamsini kwa hamsini baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Zambia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Tanzania inatambua umuhimu wa kugharamia matengenezo ya reli ya TAZARA na ndiyo maana inaendelea na jitihada za kukamilisha marekebisho ya Sheria Na. 4 ya mwaka 1995 ambayo kukamilika kwake kutaondoa changamoto zinazoathiri uwekezaji katika reli hiyo kwani uwekezaji unaofanyika sasa hauongezi thamani ya hisa za nchi inayowekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwepo kwa changamoto hiyo, Serikali ya Tanzania imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha kuwa TAZARA inaendelea kutoa huduma wakati jitihada za marekebisho ya sheria zikiendelea. Kwa mfano, katika bajeti ya mwaka 2017/2018 Serikali ya Tanzania iliipatia TAZARA jumla ya shilingi bilioni Kumi kwa ajili ya ununuzi wa vipuri vya kutengenezea vichwa saba vya treni na vifaa vya kuongeza uwezo mgodi wa mawe na kiwanda cha kutengenezea mataruma ya zege vilivyopo Kongolo Mkoani Mbeya.

Mheshimiwa Naibu Spika, vipuri na mashine hizo vimeshanunuliwa na matengenezo ya injini yamekamilika mwaka 2020 na hivi sasa zinafanya kazi. Mashine kwa ajili ya Kongolo zinafanya kazi pia. Aidha, Serikali ya Tanzania inaendelea kulipa mishahara ya wafanyakazi wa TAZARA upande wa Tanzania ambapo katika Bajeti ya mwaka 2021//2022 zimetengwa jumla ya shilingi bilioni 14.98.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumaini ya Serikali kuwa mchakato wa kurekebisha Sheria ya TAZARA utaisha hivi karibuni baada ya Serikali ya Zambia kukamilisha zoezi linaloendelea la uteuzi wa viongozi katika ngazi mbalimbali na kuwa tayari kwa kikao cha pande zote mbili kwa ngazi ya Makatibu Wakuu na hatimaye Mawaziri ili kuridhia mapendekezo ya marekebisho ya Sheria tunayoyasubiri. Ahsante.