Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 6 Health and Social Welfare Wizari wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto 76 2021-09-07

Name

Norah Waziri Mzeru

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DENNIS L. LONDO K.n.y. MHE. NORAH W. MZERU aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka mashine za incubator za kutosha nchini ili kuzuia vifo vya watoto?

Name

Dr. Dorothy Onesphoro Gwajima

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru kwa kuwa na utashi wa kuangalia afya za watoto wachanga katika Taifa letu kama sehemu ya changamoto tuliyonayo sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali lake kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kifaa cha incubator hutumika kuwasaidia watoto wachanga waliozaliwa kabla ya wakati au wenye uzito pungufu ili kuwapatia joto na kuzuia wasipoteze maisha. Hadi sasa tuna incubators 214 nchi nzima kwenye hospitali mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo tafiti zimeonesha kuna changamoto nyingi sana za kutumia incubators kuliko faida zenyewe. Incubators zimesababisha kusambaa kwa magonjwa kutoka mtoto mmoja kwenda kwa mwingine atakayefuatia kulazwa hapo. Aidha, hakuna ukaribu wa mama aliyejifungua na mtoto aliyewekwa kwenye incubator.

Mheshimiwa Spika, matumizi ya incubator katika mazingira ambayo umeme siyo wa uhakika nayo inakuwa changamoto. Hivyo, katika mazingira hayo, incubator inaweza kuwa chanzo cha uambukizo na vifo badala ya kusaidia. Hata hivyo incubators chache zilizopo zinatumika kwa ajili ya watoto waliozaliwa na uzito pungufu sana (extreme low birth weight) kwa kuzingatia kanuni za usafi wa hali ya juu.

Mheshimiwa Spika, hivyo, Wizara inasisitiza kuwa kila hospitali ianzishe vyumba maalum kwa ajili ya matibabu ya watoto wachanga ili kuendana na mwongozo wa Kitaifa wa Matibabu ya Watoto Wachanga. Vyumba hivyo ni chumba cha huduma ya Mama Kangaroo, yaani mtoto anakaa na mama kifuani kwake muda mwingi kwa watoto waliozaliwa na uzito pungufu, lakini pia na chumba cha matibabu ya mtoto mchanga mgonjwa. Kufikia Julai, 2021, jumla ya hospitali 159 zilishaanzisha vyumba hivyo na kazi inaendelea kwenye hospitali nyingine. Ahsante.