Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 59 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 491 2021-06-25

Name

Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Primary Question

MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza: -

Je, ni lini Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio itatambuliwa rasmi na kuanza kuwahudumia wananchi?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MITAA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi, Mbunge wa Jimbo la Ukerewe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tangazo la kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio lilitolewa tarehe 1/10/2007 na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa, Mamlaka za Wilaya Sheria Na. 7 ya mwaka 1982 kifungu cha 16 na 17.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2012/2013 Serikali iliunda timu ya wataalam kwa ajili ya kuchukua maoni ya wananchi kuufanya Mji Mdogo wa Nansio kuwa Halmashauri ya Mji. Wananchi wa kata kumi zilizopendekezwa kuunda Halmashauri ya Mji Nansio waliridhia Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio kupandishwa hadhi na kuwa Halmashauri ya Mji na mapendekezo hayo yaliwasilishwa Ofisi ya Rais-TAMISEMI na Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe mwaka 2014.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais-TAMISEMI ilipokea mapendekezo hayo na kutuma timu ya wataalam kwenda katika Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio ili kujiridhisha kama vigezo muhimu vinavyotakiwa ili kupandisha hadhi Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio vimefikiwa. Timu ilibaini kuwa Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio bado haikidhi vigezo vya kupandishwa hadhi na kuwa Halmashauri ya Mji.

Mheshimiwa Spika, vigezo zilivyokosekana ni pamoja na kutokuwa na idadi ya watu angalau 150,000, kutokuwa na eneo lenye ukubwa wa walau kilomita za mraba 300, kutokuwa na kata walau 12 na mitaa 60. Hivyo, Ofisi ya Rais- TAMISEMI iliishauri Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kuendelea kuilea Mamlaka ya Mji Mdogo wa Nansio mpaka itakapokidhi vigezo. Ahsante sana.