Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 54 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Waziri Mkuu: Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu 445 2021-06-18

Name

Neema Kichiki Lugangira

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA aliuliza: -

Je, ni kwa kiasi gani mifuko ya uwezeshaji kiuchumi iliyoanzishwa kwa lengo la kuwaondelea wananchi umasikini na kuwajengea uwezo wa kiuchumi imenufaisha wanawake wa kitanzania kutoka mikoa ya nje ya Dar es Salaam?

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCAL P. KATAMBI) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nitumie fursa hii adhimu kulishukuru Bunge lako la Jamhuri ya Muungano kwa kuwapa ruhusa Wabunge kujumuika nasi pale Mwanza katika tukio kubwa la Kitaifa la mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye alikuwa akikutana na vijana na changamoto zote za vijana zilizungumzwa na kujadiliwa. Lakini pia alitoa mwelekeo mzuri wa Kitaifa wa namna gani tutakavyoenda kutatua changamoto hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge lakini pamoja na hilo sambamba Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuratibu vizuri shughuli hiyo lakini sambamba na hilo tunaenda kwa kweli kupitia Waheshimiwa Wabunge hawa kuwasaidia vijana wote nchi nzima hasa kwa kuwasikiliza, kuwapokea na kutatua changamoto zao katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zaidi katika kufanya hivyo kwa kweli tutahakikisha kwamba vijana hawa wanapewa kila wanachostahili kwa Serikali kutengeneza mazingira wezeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa muda huo lakini pia sasa nitumie fursa hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia mwezi Desemba, 2020, mifuko na programu za uwezeshaji zimetoa mikopo, ruzuku na dhamana yenye thamani ya shilingi trilioni
4.34 kwa wajasiriamali 6,037,462. Kati ya hao, wanawake ni 3,079,105 sawa na asilimia 51 na wanaume ni 2,958,357 sawa na asilimia 49. Aidha, jumla ya ajira 10,844,589 zimetengenezwa kupitia uwezeshaji huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya wanawake 3,079,105 walionufaika na mikopo, ruzuku na dhamana kupitia mifuko na Programu za Uwezeshaji, wanawake 1,046,896 sawa na asilimia 34 wametokea Mkoa wa Dar es Salaam na wanawake 2,032,209 sawa na asilimia 66 wametokea katika mikoa mingine nje ya Mkoa wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi litaendelea kuweka mikakati ambayo itaimarisha utendaji wa mifuko na programu hizi ili iweze kufanya kazi kwa ufanisi na tija.