Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 52 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 430 2021-06-16

Name

Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Primary Question

MHE. NICODEMUS H. MAGANGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza barabara zote mbovu zilizopo katika Jimbo la Mbogwe?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicodemus Henry Maganga, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mbogwe lipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe lina mtandao wa barabara wenye urefu wa kilomita 1,344.3. Serikali imekuwa ikifanyia matengenezo ya barabara mbovu, pamoja na matengenezo ya kawaida kwa barabara zenye hali nzuri kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika mwaka wa fedha 2019/2020, Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe iliidhinishiwa shilingi bilioni 1.30 kwa ajili ya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 78.6, makalvati mistari 27, boksi kalvati moja pamoja na ujenzi wa barabara ya Mang’ombe – Magetini mpaka Kona nne, yenye urefu wa kilometa 1.2. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, jumla ya shilingi bilioni 1.64 ziliidhinishwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 46.6, makalvati mistari 18 pamoja na ujenzi wa barabara ya Masumbwe – Iponya yenye urefu wa kilometa moja kwa kiwango cha lami na barabara ya Mang’ombe, Magetini – Kona nne, yenye urefu wa kilomita 0.8 kwa kiwango cha lami, ujenzi wa barabara hizo umekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, Katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi bilioni 1.14 kwa ajili ya matengenezo ya barabara yenye urefu wa kilometa 74.96, Mtaro wa mawe kilometa 1.2 na ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa moja kwa kiwango cha lami katika Mji wa Masumbwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matengenezo yaliyofanyika katika mwaka wa fedha 2019/2020 na 2020/2021, yamejumuisha barabara muhimu zilizokuwa mbovu katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe, zikiwemo barabara ya Shenda - Mwabomba yenye urefu wa kilometa 17, barabara ya Isebya-Lwamgas yenye urefu wa kilometa 10. Barabara ya Ushirika-Kadoke-Ntono yenye urefu wa kilomita 5.5, barabara ya Ikunguigazi – Isabya - Nyashinge yenye urefu wa kilometa 15, barabara ya kanegere – Prison-Nyakasaluma- Bunyihuna yenye urefu wa kilometa 19.46, barabara ya Ishigamva-Busabaga-Ilolangu yenye urefu wa kilometa 15 na barabara ya Ilolangu -Kisumo-Bukombe boda yenye urefu wa kilomita 17.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe, ili kuhakikisha zinapitika katika majira yote ya mwaka na kuwezesha huduma za usafiri na usafirishaji.