Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 48 Enviroment Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano 397 2021-06-09

Name

Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-

(a) Je, Serikali imejipangaje kukabiliana na wizi wa vyuma unaosababishwa na kushamiri kwa biashara ya chuma chakavu nchini?

(b) Je, Serikali haioni kwamba biashara ya vyuma chakavu ni hatarishi hata kwa usalama wa raia na mali zao?

Name

Hamad Hassan Chande

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kojani

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004, kupitia vifungu vya 133 hadi139, Serikali imeweka kanuni za udhibiti wa taka hatarishi ikihusisha ukusanyaji, usafirishaji na uhifadhi wa taka hizo. Sambamba na uwepo wa kanuni, Serikali imekuwa ikitoa miongozo mbalimbali pamoja na elimu kwa jamii katika ulinzi wa miundombinu. Aidha, Serikali kupitia Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa kushirikiana na jeshi la polisi imekuwa ikifanya ukaguzi wa mara kwa mara katika viwanda ili kudhibiti suala la uhujumu wa miundombinu ya Serikali na watu binafsi.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, biashara ya vyuma chakavu imesaidia kuziondoa taka hizi katika mazingira na hivyo kutengeneza mazingira safi na salama kwa afya ya binadamu. Aidha, vyuma chakavu ni malighafi ya viwanda hasa viwanda vya nondo na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali imekuwa ikifanya ufuatiliaji ili kudhibiti hujuma ya miundombinu ya Serikali na watu binafsi. Aidha, wananchi na vyombo mbalimbali vinaombwa kushiriki kwa pamoja katika kulinda miundombinu dhidi ya watu waovu na wale watu wasio na uzalendo, ahsante.