Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 44 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Waziri Mkuu: Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu 367 2021-06-04

Name

Vedastus Mathayo Manyinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Musoma Mjini

Primary Question

MHE. VEDASTUS M. MANYINYI aliuliza:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani mahususi wa kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana wanapomaliza vyuo vikuu?

(b) Je, ni kwa nini vijana hao wasitumie vyeti vyao kama dhamana kupata mikopo ili wajishughulishe na shughuli mbalimbali za kiuchumi?

Name

Ummy Hamisi Nderiananga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WATU WENYE ULEMAVU alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri Mkuu, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Vedastus Mathayo Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini, lenye sehemu
(a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana wanapomaliza Vyuo Vikuu, Serikali imeandaa Mkakati wa Kitaifa wa Kukuza Fursa za Ajira ambao unatoa maelekezo kwa sekta zote za kiuchumi ya namna ya sekta hizo zinavyopaswa kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji ili wawekeze na kuzalisha fursa za ajira za kutosha. Mikakati mingine ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanzisha na kutekeleza programu ya mafunzo ya uzoefu wa kazi kwa wahitimu (internship program). Katika kipindi cha miaka mitatu jumla ya wahitimu 5,975 wamewezeshwa kupata mafunzo ya uzoefu wa kazi katika taasisi mbalimbali za Umma na binafsi ikiwa ni mkakati wa kuondoa kikwazo cha uzoefu kwa vijana wanapotafuta kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali imeanzisha na kutekeleza programu ya mafunzo ya ufundi na stadi katika fani mbalimbali kwa vijana wakiwemo wahitimu wa elimu ya juu ambapo katika kipindi cha miaka mitatu jumla ya vijana 28,941 wamepatiwa mafunzo ya ujuzi na stadi za kazi kupitia mafunzo ya uanagenzi.

Mheshima Naibu Spika, vile vile Serikali imeanzisha na kutekeleza programu ya mafunzo na kurasimisha ujuzi uliopatikana nje ya mfumo usio rasmi wa mafunzo kwa lengo la kuwawezesha vijana kuajiriwa na kujiajiri; na pia kujiendeleza kiujuzi katika taasisi mbalimbali za mafunzo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia imeanzisha na kutekeleza Programu ya Mafunzo ya Kilimo cha Kisasa kwa vijana wakiwemo wahitimu wa elimu ya juu kupitia teknolojia ya kitalu nyumba (greenhouse).

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali vile vile imeanzisha na kutekeleza programu ya vijana kufanya mafunzo katika nchi ambazo zimepiga hatua katika kilimo ambapo takribani vijana 136 wameweza kuhudhuria mafunzo ya kilimo cha kisasa nchini Israeli. Pia, Serikali imeendelea na mkakati wa pamoja wa ajira kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – Utumishi na Wizara nyingine na hasa kupitia Miradi ya Maendeleo. Vilevile Serikali imeanza kufanya utafiti kuhusu Hali ya Rasilimali watu Nchini (Manpower Survey) na utafiti wa Hali ya Ajira Nchini (Labour Force Survey).

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inapokea ushauri Mheshimiwa Mbunge wa kutumia vyeti vya uhitimu mafunzo kama dhamana ya mikopo kwa vijana na kwenda kufanyia kazi. Aidha, Serikali imeendelea kuboresha huduma ya utoaji mikopo kwa vijana kupitia mifuko na programu mbalimbali za uwezeshaji wananchi kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)