Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 40 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 340 2021-05-31

Name

Mariamu Ditopile Mzuzuri

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM D. MZUZURI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za viongozi waandamizi wa Serikali kama Makatibu Wakuu na Mawaziri katika Mji wa Dodoma kwa ajili ya makazi ya viongozi hao?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Ditopile Mzuzuri, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tangu Serikali kuhamishia shughuli zake makao makuu ya Serikali hapa Jijini Dodoma kumekuwepo na juhudi mbalimbali ili kuhakikisha kuwa viongozi waandamizi wa Serikali wanapata makazi bora ya kudumu na yenye usalama. Katika kutekeleza hilo, Serikali imeanza mkakati wa kujenga nyumba za viongozi katika jiji la Dodoma.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha 2020/ 2021 Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi - Sekta ya Ujenzi, imetenga kiasi cha shilingi bilioni sita kwa ajili ya ujenzi wa nyumba 20 za viongozi na shilingi bilioni nne kwa ajili ya ukarabati wa nyumba 40 za viongozi jijini Dodoma. Hivi sasa kwa kutumia Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) hatua za ubunifu na usanifu wa nyumba hizo pamoja na makadirio ya gharama za ujenzi zimekamilika. Aidha, ukarabati wa nyumba za viongozi jijini Dodoma unaendelea.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi - Sekta ya Ujenzi, imetenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa nyumba 20 za viongozi jijini Dodoma. Aidha, pamoja na ujenzi wa nyumba hizi, Serikali pia imetenga fedha kwa ajili ya kuendelea na ukarabati wa nyumba nyingine 40 za viongozi zilizopo jijini Dodoma katika maeneo ya Kisasa, Area D na Kilimani. Ahsante.