Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 41 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 349 2021-06-01

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO K.n.y. MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA aliuliza:-

(a) Je, nini sababu ya barabara ya Kibiti – Lindi kuharibika mara kwa mara licha ya kufanyiwa ukarabati?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatiza hilo ili kuzuia ajali za mara kwa mara katika barabara hiyo?

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anastazia James Wambura, Mbunge Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kibiti – Lindi kwa sasa inabeba magari mengi na yenye uzito mkubwa zaidi ya ilivyokusudiwa wakati wa usanifu uliotumika kujenga barabara hiyo. Hali hiyo inatokana na uwekezaji mkubwa wa viwanda na migodi katika Mikoa ya Kusini na Nyanda za Juu Kusini uliojitokeza miaka ya hivi karibuni baada ya ujenzi wa barabara hii kukamilika. Aidha, ujenzi wa viwanda vikubwa kama cha Dangote, Mkoani Mtwara na uwepo wa migodi mikubwa ya Makaa ya Mawe, Mkoani Ruvuma kumechangia ongezeko la magari yanayobeba uzito mkubwa kuliko ilivyotarajiwa wakati barabara hii inafanyiwa usanifu.

Mheshimiwa Spika, ili kukabiliana na changamoto hiyo kwa sasa, Serikali inaendelea na mpango wa ukarabati mkubwa utakaowezesha barabara hiyo kustahimili wingi na uzito wa magari kwenye barabara hii. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 jumla ya shilingi milioni 7,500 zimetengwa kwa ajili ya kazi hiyo. Aidha, pamoja na juhudi za Serikali zinazoendelea, ninaomba nitoe wito kwa wasafirishaji kutumia Bandari ya Mtwara ambayo upanuzi wake umekamilika na hivyo kuwa na uwezo wa kupokea meli nyingi na kubwa kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Spika, kutumia bandari hii ya Mtwara itasaidia sana kupunguza usafirishaji wa mizigo mikubwa kwa njia ya barabara na hivyo kunusuru barabara hiyo kuharibika mara kwa mara.