Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 39 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 325 2021-05-28

Name

Jacquline Andrew Kainja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JACQUELINE K. ANDREW aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itamaliza migogoro ya ardhi katika mikoa ya Tabora na Singida ili wananchi waweze kufanya shughuli zao kwa utulivu na amani?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Kainja Andrew, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, natambua kuwa imekuwepo migogoro ambayo kwa muda mrefu haikuwa imepatiwa ufumbuzi. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Wizara iliagiza Ofisi zote za Ardhi za Mikoa nchini ikiwemo Singida na Tabora kuanzisha jedwali la migogoro ya ardhi ili kuibainisha na kuitatua. Kwa Mkoa wa Tabora, jumla ya migogoro 211 iliorodheshwa na kati ya hiyo migogoro 102 ilipatiwa ufumbuzi. Aidha, kwa Mkoa wa Singida jumla ya migogoro 226 imetambuliwa na kati ya hiyo migogoro 34 imetatuliwa na iliyobaki asilimia 85 inatokana na madai ya fidia ambayo wananchi wanadai Halmashauri na taasisi mbalimbali za Serikali.

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Wizara katika kupunguza au kumaliza kabisa tatizo la migogoro ya ardhi nchini ni pamoja na kuongeza kasi ya upangaji, upimaji na umilikishaji ardhi kwa wananchi, kuzitaka taasisi za umma kulipa fidia kwa wananchi kwa wakati, kuendelea kutoa elimu kwa umma, kushirikiana na Serikali za mitaa kudhibiti ujenzi kwenye miundombinu ya umma kama shule, viwanja vya michezo, maeneo ya wazi, Wizara za Kisekta kushughulikia kero za makundi mbalimbali ya watumiaji ardhi kama wafugaji na wakulima na maeneo ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa wadau wote hasa taasisi za umma ambazo zinadaiwa fidia na wananchi inayochangia asilimia 39 migogoro yote nchini kuacha kuchukua ardhi za wananchi bila kilipa fidia na taasisi zinazodaiwa fidia kulipa mara moja vinginevyo maeneo hayo yatarejeshwa kwa wananchi, ahsante.