Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 38 Energy and Minerals Wizara ya Madini 319 2021-05-27

Name

Cecil David Mwambe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ndanda

Primary Question

MHE. CECIL D. MWAMBE aliuliza:-

Je, nini mpango wa Serikali baada ya kukamilika kwa Mradi wa Utafiti wa Madini ya Graphite Kata ya Chiwata?

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Jimbo la Ndanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nipende kulieleza Bunge lako tukufu kuwa, Mikoa ya kusini mwa Tanzania ikiwemo Lindi na Mtwara imebarikiwa kuwa na hazina kubwa ya madini ya kinywe ambayo kitaalam inaitwa graphite ambayo ni madini ya kimkakati yanayohitajika sana duniani kwa sasa kutokana na matumizi yake kama malighafi za viwandani.

Mheshimiwa Spika, kutokana na uwepo wa hazina ya madini hayo, yapo makampuni mengi yanayomiliki leseni za utafutaji na uchimbaji madini ya kinywe katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo mikoa ya Lindi na Mtwara. Hadi sasa kwa nchi nzima kuna jumla ya leseni 68 za utafutaji, leseni 24 za uchimbaji wa kati na leseni moja ya uchimbaji mkubwa wa madini ya kinywe.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Chiwata ambayo ipo Jimbo la Ndanda, Wilayani Masasi kuna leseni mbili za uchimbaji wa kati zilizotolewa kwa Kampuni ya Volt Graphite Tanzania Limited na leseni hizo zilitolewa mwaka 2018 baada ya kuwa kampuni hiyo imekamilisha shughuli za utafiti. Na kinachosubiriwa ni Kampuni hiyo kuanza uchimbaji na hatimaye uchakataji wa madini ya kinywe katika leseni hizo.

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuona kuwa makampuni yanayomiliki leseni za utafutaji madini yanakamilisha shughuli za utafiti na kuomba leseni za uchimbaji mkubwa na wa kati. Kuwepo kwa leseni za uchimbaji wa madini katika maeneo hayo kutasababisha kuanzishwa kwa miradi ya uchimbaji ambayo italeta mapinduzi makubwa ya kiuchumi katika Sekta ya Madini.

Mheshimiwa Spika, aidha, uanzishwaji wa miradi hiyo utaiwezesha Serikali kukusanya mapato zaidi, kutoa fursa za ajira kwa Watanzania hasa wanaoishi katika maeneo yanayozunguka miradi, uhaulishaji wa teknolojia, fedha za kigeni, lakini pia na manufaa mengine kwa jamii kupitia local content pamoja na CSR.