Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 33 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 272 2021-05-21

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. RITTA E. KABATI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya wanaume, akina mama na watoto katika Hospitali ya Wilaya ya Frelimo katika Manispaa ya Iringa?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Iringa (Frelimo) imeanza kufanya kazi kama Hospitali ya Halmashauri mwezi Februari, 2012 na kusajiliwa rasmi mwaka 2013. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali iliipatia Halmashauri ya Manispaa ya Iringa shilingi milioni 400 kwa ajili ya upanuzi wa hospitali ambapo jengo la maabara na jengo la mionzi yalijengwa na kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu iliyopo katika Hospitali ya Frelimo ni pamoja na jengo la utawala, jengo la huduma za wagonjwa wa nje (OPD), jengo la huduma za maabara, jengo la huduma za mionzi, jengo la kufualia na jengo la huduma za afya ya uzazi na mtoto. Miundombinu inayokosekana katika hospitali hii ni pamoja na jengo la upasuaji, wodi za kulaza wagonjwa, jengo la kuhifadhi maiti na jengo la kutunzia dawa. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya watoto, wodi ya wanaume na wodi ya wanawake magonjwa mchanganyiko (medical ward).