Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 30 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 259 2021-05-18

Name

Issa Jumanne Mtemvu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibamba

Primary Question

MHE. ISSA J. MTEMVU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa Hati katika Mradi wa Urasimishaji kwa Wananchi wa Kata za Kibamba, Kwembe, Mbezi, Msigani, Goba na Saranga?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Issa Jumanne Mtemvu, Mbunge wa Kibamba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutekeleza Programu ya Kurasimisha na Kuzuia Makazi Yasiyopangwa Mijini, programu ambayo ilianza 2013 na inakwenda kwisha 2023 katika maeneo mbalimbali nchini. Kuanzia mwaka 2015, Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilipanua wigo wa kushirikisha sekta binafsi kufanya kazi za urasimishaji ambapo jumla ya kampuni 163 za upangaji na upimaji ardhi zilisajiliwa zimewezesha kuandaa michoro ya urasimishaji 3,832 na jumla ya viwanja 1,638,062 katika mamlaka za upangaji 134. Kampuni hizi zinafanya kazi kwa kuingia mikataba na wananchi kupitia Kamati za Urasimishaji za Wananchi Nchini na kuratibu wa mamlaka za upangaji kuchangia gharama za urasimishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata sita za Saranga, Mbezi, Goba, Kwembe, Msigani na Kibamba, jumla ya wananchi 30,216 wamechangia gharama za upangaji na upimaji kati ya wananchi 147,299 waliotegemewa kuchangia. Aidha, Kampuni za urasimishaji kwa kushirikiana na Serikali zimeandaa michoro ya Mipangomiji 384 yenye viwanja 141,881 ambapo kati ya hivyo, viwanja 8,316 vimepimwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na kutoa hati katika viwanja 8,316 ambavyo upimaji wake umekamilika katika Kata ya Kibamba, Kwembe, Mbezi, Msigani, Goba na Saranga ambapo mpaka sasa kuna jumla ya hati 1,754 zilizoandaliwa kati ya maombi 1,925 yaliyowasilishwa. Serikali pia imekwishaandaa ankara 2,889 na kusambaza kwenye mitaa ya Kata hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kuna changamoto ya wananchi kutolipa ankara zao kwa wakati ili kuchukua hati zilizoandaliwa. Hivyo tunawasihi wananchi wa maeneo hayo kulipia gharama za umilikishwaji ili waweze kupewa hatimiliki. Vilevile kampuni zilizopewa kazi ya urasimishaji kukamilisha kwa wakati kazi walizopewa kwa kuzingatia mwongozo wa urasimishaji uliotolewa na Wizara. Ahsante.