Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 27 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 233 2021-05-11

Name

Daniel Awack Tlemai

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. DANIEL A. TLEMAI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua mgogoro wa Wananchi wa Bugeli na Hifadhi ya Manyara pamoja na mauaji ya Wananchi yanayotokea mara kwa mara?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Tlemai Awack, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Bugeli, hasa wafugaji wanapoingiza mifugo hifadhini na kukamatwa na Askari wa Hifadhi, wamekuwa na tabia ya kukataa kutii sheria bila shuruti na kupiga yowe maalum ijulikanayo kama “hayodaa” ikiwa ni kiashiria cha hatari kubwa kwa kabila la Kiiraki. Hivyo, baada ya yowe hiyo kupigwa, wananchi wengi hupata morali na kujitokeza wakiwa na silaha za jadi zikiwemo fimbo, mishale, mapanga na mikuki ili kupinga ukamataji huo wa mifugo na kuchukua mifugo yao kwa kutumia nguvu.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kumekuwepo na baadhi ya matukio ya Askari kunyang’anywa silaha au mifugo iliyokamatwa hifadhini na wananchi ambapo husababisha kutokuelewana kati ya Askari wa Hifadhi na wananchi. Pamoja na taharuki hizo, kumekuwepo pia na mauaji ya Askari wapatao wawili na majeruhi kwa Askari watatu katika eneo hilo. Aidha, matukio kama haya yamekuwa yakijitokeza katika maeneo mengine yanayozunguka hifadhi mbalimbali hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiunda Kamati mbalimbali kuchunguza matukio hayo ili kubaini chanzo cha changamoto hizo. Kwa ujumla, imebainika kuwa tatizo kubwa ni wananchi kutoheshimu makubaliano ambayo yamekuwa yakifanywa mara kwa mara kati ya Uongozi wa Wilaya, Hifadhi, Serikali ya Kijiji na wananchi kuhusu taratibu za kufuatwa na wananchi hao pindi wao wenyewe au mifugo yao inapokamatwa ndani ya hifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imedhamiria kwa dhati kuleta mahusiano mazuri kati ya wananchi na maeneo ya hifadhi kwa kuchukua hatua mbalimbali, zikiwemo kufanya vikao vya kutafuta suluhu pamoja na kupanga matumizi bora ya ardhi katika maeneo husika. Katika kutekeleza azma hiyo, Wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali itahakiki mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ziwa Manyara na kuandaa Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi kwa Kijiji cha Bugeli. Utekelezaji wake kwa sasa upo katika hatua za kukabidhi hati kwa wananchi wa kijiji husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa rai kwa wananchi wanaopakana na maeneo yaliyohifadhiwa kuepuka uvunjifu wa sheria za nchi na za uhifadhi na hivyo kudumisha amani kwa jamii husika na Taifa kwa ujumla.