Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 26 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 222 2021-05-10

Name

Dennis Lazaro Londo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mikumi

Primary Question

MHE. DENNIS L. LONDO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha wananchi wanaoishi kwenye vijiji vinavyopakana na hifadhi pamoja na mali zao wanakuwa salama kwani wanyamapori wamekuwa wakiingia na kufanya uharibifu kwenye vijiji?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, naomba kutoa pole kwa Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Mikumi kwa kadhia hiyo ya kupambana na changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu katika maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vinavyozunguka hifadhi za wanyamapori nchini vinakabiliwa na changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu kama vile tembo, simba, fisi, nyati, viboko na mamba. Pamoja na mambo mengine, hali hii hii inasababishwa na kuvamiwa kwa maeneo ya kinga (buffer zone) na mapito ya wanyamapori.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kupambana na wanyamapori wakali na waharibifu, Serikali imeunda kikosi maalum ambacho kimekuwa kikishirikiana na wadau mbalimbali kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu katika maeneo yanayozunguka hifadhi kwa kadri taarifa za matukio zinavyopatikana. Aidha, Serikali imeandaa mpango mkakati wa kitaifa wa kushughulikia wanyamapori wakali na waharibifu unaotoa mwongozo wa namna nzuri ya kuwawezesha wananchi kutumia maeneo yao bila kuathiriwa na uwepo wa wanyamapori.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati hiyo ni pamoja na kutoa mafunzo kwa wananchi wanaoishi maeneo ya pembezoni mwa hifadhi kuhusu mbinu bora za kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu. Mafunzo haya ni endelevu na yatafanyika katika maeneo yote yenye changamoto hapa nchini. Pili, kuimarisha vikosi vya doria za kudhibiti wanyamapori vikiwemo vitendea kazi ili viweze kufanya doria ipasavyo. Tatu, kushirikiana na Halmashauri za wilaya na vijiji, ili kuwezesha uandaaji wa mipango ya matumizi bora ya ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe rai kwa wananchi wa Mikumi na maeneo mengine yanayozunguka hifadhi waendelee kutoa ushirikiano na kuendelea kufuata maelekezo ya wataalam wa wanyamapori kwa kutekeleza mbinu mbalimbali za kukabiliana na wanyamapori hao ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.