Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 26 Energy and Minerals Wizara ya Madini 219 2021-05-10

Name

Boniphace Nyangindu Butondo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kishapu

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza:-

Je, ni kwa nini Mgodi wa Mwadui Williamson Diamond Limited umesimamisha shughuli za uzalishaji wa almasi kwa muda mrefu na ni lini mgodi huo utaanza uzalishaji tena?

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Nyangindu Butondo, Mbunge wa Jimbo la Kishapu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mgodi wa Mwadui unaomilikiwa na Kampuni ya Williamson Diamond Limited ulisimamisha shughuli za uzalishaji mwezi Aprili, 2020 na hii ni kutokana na kushindwa kumudu gharama za uzalishaji kufuatia anguko la bei ya madini ya almasi katika masoko ya dunia. Anguko la bei ya almasi katika soko la dunia lilisababishwa na athari za ugonjwa wa COVID-19 mwishoni mwa mwaka 2019. Athari ya kuanguka kwa bei hii ya almasi kulisababisha bei ya wastani ya almasi katika mauzo ya mgodi huo kwa mwezi Machi, 2020 kuanguka hadi kufikia Dola za Kimarekani 131.13 kwa karati, bei ambayo kimsingi haikidhi gharama za uzalishaji wa mgodi huo. Kwa mujibu wa makadirio ya mgodi huo wastani wa bei unapaswa kuwa angalau Dola za Kimarekani 208 kwa karati ili mgodi uweze kukidhi gharama za uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mgodi huo utaanza tena uzalishaji baada ya maombi yao ya overdraft funds kukubalika na benki za hapa nchini. Hii ni kwa ajili ya kugharamia shughuli zao za uzalishaji angalau kwa kipindi cha miezi mitatu hadi kufikia awamu nyingine ya mauzo ya almasi. Hali ya bei ya almasi kwenye soko la dunia kwa sasa inatarajiwa kuwa bora zaidi ikilinganishwa na kipindi cha mwaka 2020.