Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 23 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 192 2021-05-05

Name

Jesca Jonathani Msambatavangu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Iringa Mjini

Primary Question

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itarekebisha tatizo la Hospitali ya Frelimo ambayo inapata mgao kama Kituo cha Afya wakati ni Hospitali ya Wilaya ya Iringa tangu mwaka 2013?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca Jonathani Msambatavangu, Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vituo vya kutolea huduma za afya nchini ikiwemo Hospitali za Halmasahuri hupatiwa mgao wa fedha za ruzuku kwa ajili ya uendeshaji na ununuzi wa dawa na vitendanishi na vifaa tiba kwa kuzingatia vigezo maalum vilivyowekwa. Vigezo hivyo ni pamoja na idadi ya watu wanaopata huduma katika eneo husika, umbali kilipo kituo, pamoja na idadi ya vifo vya watoto chini ya miaka mitano katika Halmashauri husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, utofauti wa mgao baina ya vituo vya kutolea huduma za afya ikiwemo Hospitali ya Frelimo na Hospitali nyingine za Halmashauri hutokana na vigezo hivyo. Hospitali ya Manispaa ya Iringa Frelimo ilisajiliwa tarehe 25 Julai, 2013 kama Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Iringa na ilianza kupokea mgao wa ruzuku ya fedha za uendeshaji kama Hospitali kuanzia Agosti, 2013 ambapo kwa mwaka huu wa fedha mpaka Machi imepokea kiasi cha shilingi 53,32.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu iliyopo katika Hospitali ya Frelimo ni pamoja na jengo la Utawala, jengo la Huduma za Wagonjwa wa Nje, jengo la huduma za Maabara, jengo la huduma za Mionzi, jengo la Ufuaji na jengo la Huduma za Afya ya Uzazi na Mtoto. Miundombinu inayokosekana katika Hospitali hii ni pamoja na jengo la upasuaji, Wodi za kulaza wagonjwa, jengo la kuhifadhia maiti, na jengo la kutunzia dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuongeza majengo kwenye Hospitali hii ili kuboresha huduma zinazotolewa. (Makofi)