Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 21 Energy and Minerals Wizara ya Madini 176 2021-05-03

Name

Hawa Mchafu Chakoma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAWA M. CHAKOMA aliuliza: -

Je, ni kwa kiasi gani Serikali inafahamu madhara yatokanayo na madini ya zebaki?

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma (Mbunge wa Viti Maalum) kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, Serikali inatambua madhara makubwa ya kiafya kwa binadamu, mimea na mazingira yanayosababishwa na matumizi ya kemikali ya zebaki na hasa katika shughuli za uchenjuaji wa madini. Na miongoni mwa madhara ya kemikali hiyo kwa binadamu, ni kuathiri mifumo ya fahamu, uzazi, upumuaji na kusababisha magonjwa mbalimbali kama vile ya figo, moyo na saratani. Aidha, kemikali hiyo pia, huathiri viumbe hai vya majini na nchi kavu pindi zebaki inapotiririka na kuingia kwenye vyanzo vya maji ambavyo hutumiwa kwa matumizi mbalimbali ikiwa ni pamoja na shughuli za kibinadamu.

Mheshimiwa Spika, na njia zinazopelekea kemikali ya zebaki kuingia mwilini ni kushika, kuvuta hewa na kula vyakula vyenye viambata vya kemikali hiyo. Pamoja na athari hizo kiafya, matumizi ya zebaki katika uchenjuaji wa dhahabu yameonesha uwezo mdogo wa kutoa dhahabu ambao ni chini ya asilimia 30, hali ambayo imekuwa ikipelekea wachimbaji wadogo kushindwa kuzalisha kiwango cha kutosha na hivyo kupata faida kidogo.

Mheshimiwa Spika, ili kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali imekuwa ikitoa elimu kwa wachimbaji wadogo kuhusu athari za kemikali hiyo na kutoa njia salama za utumiaji, ikiwa ni pamoja na usakafiaji wa mialo na utumiaji wa retorts kiswahili chake ni (vigida) wakati wa uchomaji. Aidha, Serikali kupitia STAMICO itaendelea kutoa elimu ya matumizi ya njia mbadala ya uchenjuaji dhahabu kupitia vituo vyetu vya mfano vilivyoko maeneo ya Lwamgasa, Katente pamoja na Itumbi. Nakushukuru.