Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 18 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 150 2021-04-28

Name

Cecilia Daniel Paresso

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CECILIA D. PARESSO aliuliza:-

Wananchi wanaoishi jirani na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Wilayani Karatu kwa muda mrefu wamekuwa wakipata adha kubwa ya wanyama kuingia na kuvamia mashamba yao na wakati mwingine kujeruhi wananchi:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kumaliza tatizo hilo?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na shughuli za kibinadamu zikiwemo kilimo na ufugaji kwenye shoroba za wanyama, maeneo ya mtawanyiko wa wanyamapori na maeneo ya kinga ya Hifadhi ya Ngorongoro, kumekuwepo na changamoto ya wanyamapori kuingia kwenye mashamba yaliyopo pembezoni mwa hifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kukabiliana na changamoto hii, Wizara inatoa rai kwa wananchi kutumia mbinu mbadala za kuepuka wanyamapori wakali na waharibifu kuingia kwenye maeneo yao. Mbinu hizo ni pamoja na kwanza, ni kuanzisha miradi ya ufugaji nyuki kwenye mipaka ya Hifadhi zilizo karibu na maeneo ya vijiji ili kuhakikisha kuwa wanyamapori hawavuki kwenda kwenye mashamba hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbinu nyingine ni wananchi wanahamasishwa kulima zao la pilipili kandokando ya mashamba yao, kwani zao hili limeonekana kuwa ni tishio kwa wanyama wakali na waharibifu kama tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbinu nyingine ni wananchi wanashauriwa kutopanda mazao yanayovutia tembo kusogea katika mashamba yao kama vile mazao yanayohusiana na katani, miwa, ndizi na matikiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile wananchi kuendelea kutumia oil chafu iliyochanganywa na pilipili na majivu ili kuzuia wanyama kama tembo kusogea kwenye maeneo ya mashamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, ni wananchi wanashauriwa sasa kutoa taarifa haraka pindi wanyama hao wanapoonekana kukaribia kwenye maeneo ya mashamba.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto za kuongezeka kwa matukio mbalimbali ya wanyama wakali wakiwemo tembo, Wizara imeongeza idadi ya vituo vya muda na vya kudumu vya askari katika maeneo yaliyohifadhiwa likiwemo eneo la Ngorongoro (Wilaya ya Karatu) na kuendelea na doria za usiku kuhakikisha wanyamapori waharibifu wanarudishwa hifadhini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)