Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 18 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 148 2021-04-28

Name

Bonnah Ladislaus Kamoli

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Segerea

Primary Question

MHE. BONNAH L. KAMOLI aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali itaongeza Vituo vya Afya katika Kata za Jimbo la Segerea Pamoja na kupandisha hadhi Zahanati za Kinyerezi, Segerea, Kipawa na Yombo Kiwalani ili kuondoa adha kwa wananchi wa Kata 13 wanaotegemea Kituo kimoja cha Afya?

(b) Je, ni lini Kata za Minazi Mirefu, Buguruni, Kimanga na Kisukuru zitapatiwa Zahanati?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bonnah Ladislaus Kamoli, Mbunge wa Segerea, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha huduma za afya katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali iliipatia Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam; iliyokuwa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Mwezi Februari 2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tatu kwenye Hospitali ya Halmashauri na imeitenga shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2020/ 2021 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 na 2019/2020, Serikali iliipatia Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam shilingi bilioni moja kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Guluka Kwalala na upanuzi wa Kituo cha Afya Buguruni.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kupitia mapato yake ya ndani, imetenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vitatu vya afya na shilingi bilioni 2.7 kwa ajili ya kuongeza miundombinu katika zahati tano ili ziweze kupandishwa hadhi kuwa vituo vya afya zikiwemo Zahanati za Kinyerezi na Kiwalani katika Jimbo la Segerea.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 250 kwa ajili ya kukamilisha maboma matano ya zahanati katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam zikiwemo Zahanati za Bonyokwa na Tabata zilizopo katika Jimbo la Segerea. Aidha, kupitia mapato ya ndani, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imetenga shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kulipa fidia kwenye maeneo ambayo yatachukuliwa na Serikali kwa ajili ya ujenzi na upanuzi wa vituo vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu ya huduma za afya katika Jimbo la Segerea na nchini kote ili kuendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi. (Makofi)