Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 16 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 138 2021-04-23

Name

Jacquline Andrew Kainja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JACQUELINE K. ANDREA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italiangalia zao la asali na kulitafutia soko la uhakika ndani na nje ya nchi?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Kainja Andrea, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, asali ni mojawapo ya mazao yanayozalishwa na nyuki, mazao mengine ni pamoja na nta, gundi ya nyuki, sumu ya nyuki, chavua na maziwa ya nyuki. Wizara imeendelea na jitihada za kutangaza mazao ya nyuki ya Tanzania kwa kushirikiana na TANTRADE kwenye mikutano mbalimbali ya kibiashara, maonyesho, warsha na makongamano yanayofanyika ndani na nje ya nchi pamoja na Balozi zetu zilizopo katika nchi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa uzalishaji wa asili nchini ni wastani wa tani 30,400; sehemu kubwa ya asali hiyo zaidi ya asilimia 95 huuzwa katika soko la hapa nchini na asilimia tano huuzwa kwenye soko la nje kwenye nchi za Rwanda, Kenya, Burundi, Umoja wa Jumuiya ya Ulaya na Umoja wa Nchi za Kiarabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na ukarabati pamoja na ujenzi wa viwanda vya kuchakata mazao ya nyuki katika Mikoa ya Tabora, Katavi, Kigoma na Geita ambavyo vitatumika kama soko la mazao ya nyuki. Serikali pia imeweka mfumo wa ufuatiliaji wa mazao ya nyuki katika mnyororo mzima wa thamani wa mazao hayo kwa lengo la kuthibiti viwango vya ubora wa mazao ya nyuki pamoja na kufufua, kuendeleza na kuhamasisha uanzishwaji wa vyama vya ushirika wa ufugaji nyuki ili kuunganisha nguvu za uzalishaji pamoja na soko la uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara itaendelea kuhakikisha upatikanaji wa soko la mazao ya nyuki kupitia mradi mpya wa kusaidia mnyororo wa thamani wa ufugaji nyuki utakaotekelezwa kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022. Naomba kuwasilisha.