Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 16 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 137 2021-04-23

Name

Charles John Mwijage

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba Kaskazini

Primary Question

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE aliuliza:-

Visiwa vilivyopo katika Ziwa Victoria, Wilayani Muleba havina usafiri salama na wa uhakika, na vilevile Bandari Ndogo ya Kyamkwikwi haina miundombinu stahili.

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kupeleka kivuko ili kurahisisha usafiri kati ya Visiwa vilivyopo Ziwa Victoria na Miji ya Mwambao ya Ziwa hilo Wilayani Muleba?

(b) Je, ni lini Serikali itajenga miundombinu muhimu ikiwemo maghala ya kuhifadhia bidhaa katika Bandari Ndogo ya Kyamkwikwi ili kuwavutia wafanyabiashara kutumia bandari hiyo?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Charles John Mwijage, Mbunge wa Muleba Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Kwa sasa Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, Sekta ya Uchukuzi tayari imepeleka wataalam maeneo yanayozunguka Ziwa Victoria, hususan Wilaya ya Muleba kufanya tathimini ya maeneo yanayofaa kuwekewa huduma ya usafiri wa vivuko. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, Sekta ya Ujenzi, imetenga kiasi cha shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa maegesho ya Muleba – Ikuza na Ngara – Nyakiziba.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali kwa kuuona umuhimu wa huduma hiyo kwa wananchi wa maeneo hayo, inaangalia uwezekano wa kuboresha huduma za usafiri zinazotolewa na Kivuko MV Chato II – Hapa Kazi Tu, kwa kuongeza njia (route) ya kutoka Chato hadi kwenye visiwa vinavyoweza kufikiwa na kivuko hicho katika Wilaya ya Muleba.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imekamilisha zoezi la utwaaji wa ardhi katika Bandari Ndogo ya Kyamkwikwi kwa lengo la kujenga miundombinu muhimu ili kuwavutia wafanyabiashara pamoja na kutoa huduma za usafiri wa kuelekea maeneo mengine ya Ziwa Victoria kupitia Bandari hiyo. Hadi sasa kazi ya kuainisha mahitaji ya miundombinu inayofaa kujengwa katika Bandari hiyo imekamilika. Miundombinu husika ni pamoja na ghala la kuhifadhia mizigo, jengo la kupumzikia abiria, kantini na chumba cha walinzi. Utekelezaji wa mradi huu unatarajia kuanza katika kipindi cha mwaka wa fedha 2021/2022. Ahsante.