Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 16 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 130 2021-04-23

Name

Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Primary Question

MHE. MAIMUNA S. MTANDA aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali itaongeza bajeti ya barabara za Newala Vijijini ambayo imetengewa fedha za kilometa 340 wakati zina mtandao wa barabara wa kilometa 960?

(b) Je, Serikali inatoa msaada gani wa dharula kwenye matengenezo ya barabara za vijijini vinavyozungukwa na milima au mito kama vile Mkongi – Nanganga, Mikumbi – Mpanyani, Namdimba – Chiwata, Mkoma – Chimenena na Miyuyu – Ndanda?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maimuna Salum Mtanda, Mbunge wa Jimbo la Newala Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Newala ina mtandao wa barabara wenye urefu wa kilometa 960.04. Serikali imekuwa ikiongeza fedha za bajeti ya matengenezo ya barabara katika Halmashauri ya Newala mwaka hadi mwaka. Katika mwaka wa fedha 2019/2020, shilingi milioni 939.27 zilitengwa kwa ajili ya kuzifanyia matengenezo barabara zenye urefu wa kilometa 343.86, mwaka wa fedha 2020/2021, shilingi milioni 976.88 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 320.38.

Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi bilioni 1.056 kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 277.35 na ujenzi wa mifereji yenye urefu wa kilometa 1.37.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020 barabara ya Mkwiti - Lochino - Nyangao yenye urefu wa kilometa 11.1 imefanyiwa matengenezo kwa gharama ya shilingi milioni 84.78. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 barabara hii imetengewa shilingi milioni 56.32. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 87 kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Maputi – Mikumbi – Miyuyu – Ndanda Kibaoni yenye urefu wa kilometa 17.5 ikiwa sehemu ya kipande cha Mlima Miyuyu – Ndanda na shilingi milioni 56 kwa ajili ya matengenezo ya maeneo korofi yenye urefu wa kilometa 3.5 ili iweze kupitika hadi Kijiji cha Lochino.