Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 14 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 123 2021-04-21

Name

Soud Mohammed Jumah

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Donge

Primary Question

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuiwezesha Mifuko ya Kuendeleza Utalii na Wanyamapori na kufikia lengo la watalii milioni tano ifikapo 2025?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Soud Mohammed Jumah, Mbunge wa Donge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Tozo ya Maendeleo ya Utalii (TDL) ulianzishwa kwa Sheria ya Utalii Na. 29 ya Mwaka 2008, Kifungu cha 59(2). Lengo la Tozo hiyo ni kuendeleza mazao ya utalii; kudhibiti ubora wa huduma za biashara za utalii; kukuza na kutangaza vivutio vya utalii; kujenga uwezo katika sekta ya utalii; na kuwezesha tafiti na shughuli nyingine yoyote kwa ajili ya maendeleo na kuboresha sekta ya utalii.
Kutokana na mabadiliko ya Sheria ya Fedha ya Mwaka 2020, vyanzo vya tozo hii kwa sasa vinakusanywa na Wizara kwa kushirikiana na TRA na makusanyo hayo huingizwa katika Mfuko Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa wanyamapori, upo Mfuko wa Kuhifadhi Wanyamapori Tanzania ambao ulianzishwa kwa Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori Sura 283, Kifungu cha 91(2). Mfuko huo unawezesha shughuli za kuhifadhi wanyamapori ndani na nje ya maeneo ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha wanyamapori wanaendelea kulindwa na kusimamiwa kwa ajili ya kuendeleza utalii nchini, mifuko ya utalii na wanyamapori imekuwa ikiwezeshwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo. Pamoja na vyanzo vya mapato vya mifuko hii kukusanywa na kupelekwa kwenye Mfuko Mkuu (Hazina), Serikali kwa mwaka wa fedha 2021/2022 imetenga fedha kupitia bajeti kuu ya Serikali kwa ajili ya kutekeleza kazi za mifuko husika. Hivyo, kazi zilizokuwa zinafanywa na mifuko hii sasa zitatekelezwa kupitia bajeti kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.