Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 10 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 80 2021-04-15

Name

Esther Lukago Midimu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ununuzi wa Vifaa Tiba ikiwemo vya upasuaji katika Kituo cha Afya cha Mwabayanda Wilayani Maswa?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Kituo cha Afya Mwabayanda kilipatiwa shilingi milioni 400 kwa ajili ya upanuzi kwa kuwa awali ilikuwa ni zahanati. Ujenzi na ukarabati wa Kituo cha Afya Mwabayanda umekamilika na kituo kimeanza kutoa huduma za dharura za upasuaji kwa akina mama wajawazito kuanzia mwezi Oktoba 2020 baada ya kupatiwa vifaa tiba kutoka kwenye vituo vingine vilivyopo katika Mkoa wa Simiyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2020/2021, Serikali imetoa shilingi bilioni 26 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika vituo vya afya vilivyojengwa awamu ya kwanza na ya pili na vifaa vya shilingi bilioni 15 tayari vimeshapokelewa na taratibu za kupeleka vifaa vya shilingi bilioni 11 zinaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya cha Mwabayanda kilijengwa katika awamu ya nne; na hivyo vituo vyote vya afya vilivyojengwa awamu ya tatu na ya nne vitatengewa fedha ya ununuzi wa vifaa tiba katika bajeti ya mwaka 2021/2022. Aidha, naishauri Halmashauri ya Wilaya ya Maswa kupitia mapato yake ya ndani itoe kipaumbele cha ununuzi wa vifaa tiba kwa awamu ili kuboresha huduma za afya kwa wananchi wakati Serikali ikiendelea kutafuta fedha za ununuzi wa vifaa tiba.