Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 10 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 79 2021-04-15

Name

Vincent Paul Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Primary Question

MHE. VICENT P. MBOGO aliuliza:-

Jimbo la Nkasi Kusini lina Kata 11 na Kituo cha Afya kimoja pekee:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza Vituo vya Afya hasa katika Tarafa ya Chala, Kate, Myula, Sintali na Ninde?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vincent Paul Mbogo, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi, ambapo katika mwaka wa fedha 2017/2018 hadi mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imejenga na kukarabati Vituo vya Afya vya Nkomolo na Kirando kwa gharama ya shilingi milioni 900. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetoa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tatu na shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi. Vilevile, Serikali imetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma matatu ya zahanati katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kusogeza zaidi huduma za afya kwa wananchi, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi inakamilisha utaratibu wa kuingia makubaliano ya utoaji wa huduma za afya (service agreement) na Kituo cha Afya cha Mzimwa kinachomilikiwa na Taasisi ya Kikatoliki Abei kwa ajili ya wananchi kupata huduma za afya ikiwemo upasuaji wa dharura ambapo wananchi kutoka Tarafa za Myula na Sintali ni miongoni mwa watakaonufaika na mpango huo. Aidha, Halmashauri imetenga eneo katika Tarafa ya Chala kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kituo cha afya kupitia fedha za mapato ya ndani katika mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kujenga na kupanua vituo vya kutolea huduma za afya katika Jimbo la Nkasi na nchini kote kwa awamu kwa kuwa shughuli hizi ni endelevu.