Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 9 Water and Irrigation Wizara ya Maji 72 2021-04-14

Name

Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Primary Question

MHE. NICODEMUS H. MAGANGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka Wilayani Mbogwe maji kutoka Ziwa Victoria kwa ajili ya matumizi ya Wananchi?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicodemus Henry Maganga, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa Wilaya ya Mbogwe ni wastani wa asilimia 55. Huduma hiyo ya maji inapatikana kupitia miradi minne ya skimu, visima virefu 26, visima vifupi 460 na matanki 55 ya kuvuna maji ya mvua, vituo vya kuchotea maji 61 na maunganisho ya nyumbani 192.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha huduma za maji, Serikali katika mwaka wa fedha 2020/2021, ilitenga jumla ya shilingi bilioni 2.9 kwa ajili ya upanuzi wa miradi ya maji Lulembela na Nyakafuru, ujenzi wa miradi mipya ya maji Mbogwe, Nanda na Kabanga-Nhomolwa. Hadi sasa jumla ya shilingi bilioni 1.8 zimetolewa, ambapo kazi zilizofanyika ni ujenzi wa nyumba ya pampu ya kusukuma maji, matenki matano, vituo vya kuchotea maji 48 na ulazaji wa bomba lenye urefu wa kilometa 31. Utekelezaji wa miradi hiyo unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Aprili, 2021 na kuongeza upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama kufika asilimia 61 ifikapo mwezi Disemba, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali kupitia Mpango wa Mradi wa Maziwa Makuu kupitia Ziwa Victoria, katika Wilaya ya Mbogwe itatekeleza miradi katika Vijiji vya Kagera, Ilolangulu, Buningozi, Ngemo, Isungabula na Iponya.