Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 67 2021-09-07

Name

George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani kuwasaidia Wanafunzi ambao wamechaguliwa kwenda kusomea kozi ambazo hawakuzichagua katika Matokeo ya Mtihani wa Kidato cha nne yaliyotoka mwaka 2021?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais_TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Ranwell Mwenisongole, Mbunge wa Jimbo la Mbozi Kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali hutumia fomu maalum itwayo Student Selection Form (Sel-Form) ambayo humuwezesha mwanafunzi kuchagua tahasusi na kozi anazopenda kusomea endapo atachaguliwa kujiunga na kidato cha tano au vyuo vya ulimu wa ufundi, ambapo hujazwa na wahitimu wote wanaotarajia kuhitimu kidato cha nne mara baada ya kumaliza mitihani yao.

Mheshimiwa Spika, mwanafunzi anaweza kuchagua wapi anahitaji kwenda kusoma, kama ni kuendelea na masomo ya elimu ya Sekondari (kidato cha tano), vyuo vya elimu ya ufundi, vyuo vya ualimu au vyuo vya afya. Kwa kila chaguo mwanafunzi hupewa machaguo matano ya kuchagua tahasusi na shule anayohitaji kusoma au kozi na chuo anachohitaji kusoma. Endapo mwanafunzi ataridhia atapewa machaguo matano ya kozi na vyuo vya kati anavyohitaji kusoma. Wanafunzi huchaguliwa kujiunga na vyuo vya elimu ya ufundi, vyuo vya afya au ualimu endapo wamechagua kama chaguo la kwanza kwa sababu wanataka kupata ujuzi badala ya kujiunga na kidato cha tano au wamekosa nafasi ya kujiunga na kidato cha tano.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali haina mpango wa kuwagharamia wanafunzi wanaochaguliwa kusomea kozi mbalimbali katika vyuo vya kati isipokuwa wanafunzi wanaochaguliwa moja kwa moja kujiunga na vyuo vya ufundi vitatu ambavyo ni Taasisi ya Sayansi na Teknolojia Dar es Salaam (DIT), Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST).

Mheshimiwa Spika, Serikali imejikita kuongeza nafasi za kudahili wanafunzi wa kidato cha tano, hivyo idadi ya wanafunzi wanaojiunga na kidato cha tano imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka. Idadi ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano mwaka 2021 ni wanafunzi 87,663 ikilinganishwa na wanafunzi 73,113 waliochaguliwa mwaka 2020.