Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 3 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 36 2021-09-02

Name

Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ASIA A. HALAMGA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa muda mrefu wa kuwatambua na kulinda maslahi ya vijana waliojiajiri katika sanaa ya burudani kama Video Vixen na Video King?

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Asia Abdukarimu Halamga, Mbunge wa Viti Maalum, Kundi la Vijana kutoka Mkoa wa Manyara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Video Vixens na Video Kings ni walimbwende, wachezaji, waigizaji, wanamitindo au watu wengine maarufu ambao hushiriki kwenye Sanaa hasa katika muziki wa video (audio-visual) kwa lengo la kuiongezea mvuto kazi husika. Hawa hushirikishwa na wamiliki wa kazi husika kwa makubaliano maalum.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki Na. 7 ya mwaka 1999, anaepaswa kulipwa mrabaha wa kazi ya sanaa ni mtunzi, mbunifu na mtayarishaji (producer) wa kazi ya sanaa husika.

Mheshimiwa Spika, ili kuweza kuifikia na kuivutia hadhira yake, Sanaa hii imekuwa ikiwashirikisha Video Vixen na Video Kings, Serikali ilifanya marekebisho ya Sheria hii kifungu cha 47(b) mwaka 2019 ili kuipa COSOTA mamlaka ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mikataba ya kimaslahi kati ya wenye kazi hiyo ya sanaa na vijana wetu hawa.

Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa wadau wote wa sanaa ya burudani kuishirikisha COSOTA ili maslahi yao yaweze kulindwa kupitia mikataba.