Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 18 Water and Irrigation Ofisi ya Rais TAMISEMI. 150 2016-05-12

Name

Maida Hamad Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RITTA E. KABATI (K.n.y. MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH) aliuliza:-
Baadhi ya miradi ya maji inayosimamiwa na Halmashauri imekuwa ikisuasua kutokana na uchache wa fedha pamoja na kuingia mikataba na wakandarasi wasiokuwa na uwezo wa kutosha na kusababisha miradi hiyo kutokamilika kwa wakati:-
Je, Serikali imejipanga vipi kumaliza tatizo la maji kwa wananchi wa vijijini?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maida Hamad Abdallah, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika Programu ya Awamu ya Kwanza ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, Serikali ilipanga kutekeleza miradi ya maji 1,870 katika Halmashauri mbalimbali nchini. Miradi iliyotekelezwa na kukamilika ni 1,110 katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Katika bajeti ya mwaka wa fedha 2015/2016, Halmashauri zilitengewa shilingi bilioni 129.3 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji. Hadi sasa fedha zilizopelekwa kwenye Halmashauri ni shilingi bilioni 97.6 sawa na asilimia 75.5 ya fedha zilizotengwa.
Mheshimiwa Spika, changamoto ya upelekaji wa fedha za miradi ya maji katika Halmashauri, imechangiwa kwanza na kutofikiwa kwa malengo ya makusanyo ya mapato kwa mwaka na pili baadhi ya wahisani kuchelewa kutoa fedha walizoahidi. Katika bajeti ya mwaka 2016/2017, Serikali imetenga shilingi bilioni 290 ambazo zitatumika kulipa madeni ya wakandarasi na kukamilisha miradi viporo.
Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali hivi sasa ni kuimarisha makusanyo ya fedha ili fedha zilizotengwa ziende katika utekelezaji wa miradi iliyopangwa.